Wadau
wa masuala ya uchambuzi wa Afrika pamoja na baadhi ya wanasiasa
wamewataka vijana kuwa makini katika mustakabali wa nchi zao,
wakisisitiza umuhimu wa kulinda amani na kuepuka hatua zinazoweza
kuirejesha jamii katika umaskini na kudhoofisha maendeleo ya
taifa.
Wito huo umetolewa jijini Dar es Salaam wakati wa
uzinduzi wa makala maalum kuhusu matukio yaliyotokea Oktoba 29, 2025,
iliyotayarishwa na mwandishi wa habari kutoka Nigeria, David
Hundeyin, katika ukumbi wa Maktaba Mpya ya Chuo Kikuu cha Dar es
Salaam (UDSM).
Akizungumzia makala hiyo, mwanasiasa mkongwe
Hamad Rashid amesema vijana wanapaswa kutambua thamani ya taifa lao
na kujiepusha na vitendo vinavyoweza kuharibu taswira ya
nchi.
Amesema Serikali inapaswa kuendelea kuimarisha ajira kwa
vijana, akibainisha kuwa suala la ajira ni la kitaifa na linahitaji
kushughulikiwa na taasisi zote ili kulinda amani na utulivu.
“Kwenye
makala hii nimejifunza umuhimu wa kulinda amani ya nchi na Afrika kwa
ujumla. Kama kuna changamoto za haki za binadamu, zishughulikiwe kwa
kufuata taratibu sahihi ikiwemo mijadala ya Katiba mpya,” amesema
Rashid.
Naye Katibu wa Chama cha NRA, Almas Kisbya, amesema
vijana wanapaswa kuwa makini katika kufanya maamuzi na kuthamini
rasilimali za taifa lao.
“Vijana wanapaswa kujenga imani kwa
taarifa zinazotolewa ndani ya nchi badala ya kutegemea taarifa kutoka
nje pekee. Ni muhimu kuthamini taifa letu na kushiriki katika
kulijenga,” amesema Kisbya.
Kwa upande wake, mchambuzi wa
masuala ya Afrika, Joshua Maponga, amesema vijana wako katika hatari
ya kupoteza mwelekeo iwapo hawatakuwa makini.
“Baadhi ya
mataifa ya Magharibi hunufaika na hali ya misukosuko katika mataifa
ya Afrika, hivyo vijana wanapaswa kuwa makini na kulinda maslahi ya
nchi zao,” amesema Maponga.

0 Maoni