Katibu wa Itikadi, Uenezi na
Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kenani Kihongosi, amewataka
wananchi wa Wilaya ya Hanang' mkoani Manyara kutokubali kushawishiwa
kushiriki maandamano ya vurugu, akisema yanaweza kusababisha
uharibifu wa mali za umma na kurudisha nyuma jitihada za
maendeleo.
Akizungumza katika mkutano na wananchi wa Hanang',
Kihongosi alisema watu wanaochochea vurugu hawana maslahi ya wananchi
kwa kuwa athari za matukio hayo huwakumba wananchi wenyewe kupitia
uharibifu wa huduma muhimu na miundombinu ya kijamii.
Alieleza
kuwa vitendo vya kuchoma vituo vya polisi, vituo vya afya na
miundombinu mingine ya umma husababisha hasara kubwa kwa jamii na
kuathiri utoaji wa huduma muhimu zinazotegemewa na wananchi katika
maisha yao ya kila siku.
"Wanaowashawishi kushiriki
vurugu hawana maslahi na maendeleo ya wananchi. Mali zinazoharibiwa
ni za wananchi wenyewe na madhara yake huwakumba wananchi kwa
kupoteza huduma muhimu," alisema Kihongosi.
Kiongozi huyo
wa CCM aliwataka wananchi kuelekeza nguvu zao katika shughuli za
uzalishaji mali badala ya kushiriki vitendo vinavyoweza kuhatarisha
amani na utulivu wa nchi.
Alisema maandamano yenye tija kwa
wananchi ni yale yanayochochea maendeleo kupitia kufanya kazi kwa
bidii, kuongeza uzalishaji na kuboresha hali za maisha.
"Maandamano
ya maendeleo ni kufanya kazi kwa bidii, kulima, kufanya biashara na
kuendesha shughuli halali za kujiongezea kipato. Hiyo ndiyo njia
sahihi ya kuboresha maisha ya mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla,"
alisema.
Aidha, aliwasisitiza wakulima, wafanyabiashara na
waendesha bodaboda kuendelea kujikita katika shughuli zao za kiuchumi
huku wakilinda amani na mshikamano wa jamii.
Kihongosi
alihitimisha kwa kuwataka wananchi kuendelea kushiriki kikamilifu
katika shughuli za maendeleo na kulinda amani ya nchi, akisema
utulivu uliopo ni msingi muhimu wa ustawi wa familia na maendeleo ya
taifa.

0 Maoni