Tanzania na Kenya zimekubaliana kuharakisha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya njia za umeme zinazounganisha gridi za nchi hizo mbili pamoja na kuboresha mifumo ya usafirishaji wa umeme ili kuimarisha usalama wa nishati, kuongeza uhakika wa upatikanaji wa umeme na kukuza biashara ya umeme katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Makubaliano
hayo yamefikiwa baada ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati
anayeshughulikia Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Felchesmi
Mramba, kufanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na
Mafuta wa Kenya, Bw. Alex Wachira, jijini Nairobi, Kenya.
Mazungumzo hayo yalijikita katika kuimarisha ushirikiano katika sekta ndogo ya umeme na nishati jadidifu, hususan biashara ya umeme, utekelezaji wa miradi ya uunganishaji wa gridi za umeme pamoja na maboresho ya mifumo ya usafirishaji na usambazaji wa umeme kati ya Tanzania na Kenya.
Viongozi hao pia walijadili hatua mbalimbali za
kuimarisha biashara ya umeme katika ukanda wa Afrika Mashariki
kupitia Umoja wa Soko la pamoja la Kuuziana Umeme na Kuimarisha
Mifumo ya Gridi-Eastern Africa Power Pool (EAPP).
Sambamba
na hilo, Makatibu Wakuu hao walisisitiza umuhimu wa kuongeza wigo wa
njia za usafirishaji umeme zitakazounganisha nchi hizo mbili kupitia
maeneo ya Namanga, Lungalunga, Loitoktok na Isibania/Sirari.
Aidha,
kikao hicho kilijadili pendekezo la kuanzishwa kwa mfumo wa Ring
Circuit utakaojumuisha njia za Ibadakuli – Masaka, Ibadakuli –
Kilgoris na Kilgoris – Masaka kwa lengo la kuongeza uthabiti wa
gridi za umeme na kuimarisha biashara ya umeme kati ya Tanzania na
Kenya.
Katika
hatua nyingine, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Mafuta wa Kenya,
Bw. Alex Wachira alieleza kuwa nchi hiyo imejipanga pia katika
uwekezaji wa miundombinu ya gesi asilia kwa lengo la kuimarisha
upatikanaji wa nishati hiyo nchini humo, pia kuongeza ushirikiano wa
kikanda katika sekta ya nishati.
Aidha, Kenya ilieleza uzoefu wake katika biashara ya umeme wa kikanda, ikibainisha kuwa inaendelea kupokea umeme kutoka Ethiopia kupitia mikataba ya biashara ya umeme ya kikanda, ambapo kiwango cha umeme hupungua na kuongezeka kulingana na mahitaji, huku kikifikia takriban megawati 100 katika vipindi vya kawaida.
Hatua hiyo imeelezwa
kusaidia kuimarisha uthabiti wa mfumo wa umeme nchini Kenya.
Kikao hicho kilihudhuriwa na viongozi na wataalam mbalimbali kutoka Wizara za Nishati za Tanzania na Kenya pamoja na taasisi za sekta ya umeme zikiwemo TANESCO, KETRACO na KPLC.


.jpeg)
0 Maoni