Nyota ya alfajiri ing'aayo kaskazini

 

Wahenga walisema “Pori ni kitabu cha maisha, kila kipande kinasimulia hekima.” Kisha wakaongeza kusema " Palipo na uhai, pana matumaini".

Methali hizi za kale za Kiswahili zinapata maana yake kamili katika simulizi za Makuyuni Wildlife Park, Hifadhi iliyo ndani ya Halmashauri ya Monduli, Mkoa wa Arusha , ambayo kila uchwao inazidi kung’ara kama nyota ya alfajiri, ikiangaza njia mpya za  utalii na watalii  pamoja na uhifadhi endelevu nchini Tanzania.

Tarehe 11 Oktoba 2025  iligeuka kuwa ukurasa wa dhahabu katika historia ya Makuyuni. Pale ambapo Miss World China 2021, Bi Jiang Sigi, aliwasili kwa madaha, akiwa ameambatana na walimbwende  walioshinda tuzo ya Marvel Travel World kutoka Hong Kong, Tanzania, na Kenya. Wageni hawa mashuhuri wakipokelewa kwa bashasha na  tabasamu la ukarimu na maelezo ya kuvutia kuhusu utajiri wa wanyamapori wanaoifanya Makuyuni Wildlife Park kuwa hifadhi ya kipekee nchini Tanzania.

Walitembea kwenye nyasi za dhahabu za porini, wakishuhudia pundamilia wakicheza kwa furaha, swala wakikimbia kwa ustadi, nzohe wakirukaruka mithili ya sokwe mtu walioshiba makuzi ya mwanasayansi aliyeacha nyayo zisizofutika, Dkt. Jane Goodall, na twiga wakinyoosha shingo zao kuelekea mawinguni kama tausi atanuavyo mkia wake Kwa maringo. Bi Jiang Sigi alitamka kwa mshangao,

 这个地方是, 颗隐藏的宝石,是全世界都应该看到的珍宝。(Kwa lugha kichina).

Maneno yake yakitoa tafsiri ya lugha iliyokuja nchini Kwa merikebu kusema “This place is a hidden gem, a treasure the world must see.”

Siku iliyofuata, tarehe 12 Oktoba 2025, hifadhi hiyo ilipokea Kikundi cha Utalii Fitness kutokea Njiro Msola Jijini Arusha kikiongozwa na Mkufunzi wa Kuafit Gym Bw. Benson Godfrey Njiro, Arusha, kundi lenye hadhi yake katika jamii. Wakiwa wamebeba ukakamavu wa kazi yao, waliingia Makuyuni kwa lengo la mapumziko, lakini waliondoka wakiwa wameguswa na falsafa ya uhifadhi. Mmoja wao alisikika akisema "Tulikuja kama walinzi, lakini tumepigwa na butwaa kama watalii"

Kwa sasa, Makuyuni Wildlife Park imekuwa mfano hai wa hifadhi inayopokea wageni wa kila tabaka kutoka wageni wa kimataifa hadi wazawa wanaotafuta pumziko, elimu, na msisimko wa asili. Kila ujio mpya ni ushuhuda wa namna Makuyuni inavyozidi kunyanyuka, ikiimarika kama alama ya utalii endelevu na urithi wa taifa.

Makuyuni imekuwa sio tu kivutio cha watalii, bali ni kioo kinachoakisi sura halisi ya Tanzania yenye neema na utajiri wa vivutio vya utalii.

Na jua linapozama nyuma ya milima ya Monduli, anga la Makuyuni hubadilika kuwa kitambaa cha machungwa na zambarau, ishara kwamba hata giza likishuka, nyota ya Makuyuni itaendelea kung’aa kaskazini, ikitoa mwanga wa matumaini kwa uhifadhi wa taifa.



            Na Beatus Maganja - Arusha

Chapisha Maoni

0 Maoni