Ngorongoro yaendelea kuvutia wageni wengi maonesho ya Magical Kenya

 

Wageni kutoka mataifa mbalimbali wameendelea kumiminika kwenye banda la Hifadhi ya Ngorongoro katika maonesho ya kimataifa ya utalii ya Magical Kenya Travel Expo yanayoendelea jijini Nairobi, nchini Kenya, huku wengi wakivutiwa na vivutio vya pekee vinavyopatikana katika hifadhi hiyo maarufu duniani.

Katika maonesho hayo, wageni wameonyeshwa fursa mbalimbali za utalii na uwekezaji zinazopatikana ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro, huku kreta ya Ngorongoro ikivutia hisia za wengi kutokana na mandhari yake ya kipekee na uwepo wa wanyama wakubwa watano (Big Five), sambamba na historia ya kipekee ya chimbuko la binadamu wa kale.

Afisa Masoko Mkuu wa Hifadhi ya Ngorongoro, Bw. Michael Makombe, amesema ushiriki wao katika maonesho hayo umefungua milango mipya ya ushirikiano wa kimataifa na kuimarisha juhudi za kuitangaza Tanzania kama kitovu cha utalii barani Afrika.

“Ushiriki wetu katika Magical Kenya umeongeza mwamko mkubwa wa kimataifa. Wageni wengi wameonesha nia ya kutembelea Ngorongoro na tayari tumeanza kupokea maombi ya ziara kutoka kwa mawakala wa utalii wa kimataifa,” amesema Makombe.

Makombe ameongeza kuwa mbali na vivutio vya asili, historia ya binadamu wa kale inayopatikana katika Bonde la Olduvai Gorge imeendelea kuwa kivutio cha kipekee kinachotofautisha Ngorongoro na hifadhi nyingine duniani.

Maonesho ya Magical Kenya ni jukwaa muhimu la kutangaza vivutio vya utalii barani Afrika na duniani kote, yakihusisha wadau mbalimbali wa sekta ya utalii wakiwemo waendeshaji wa safari, wawekezaji, na wakala wa utalii wa kimataifa.


              Na. Hamis Dambaya – Nairobi

Chapisha Maoni

0 Maoni