Mloganzila yaendelea na kambi ya kutengeneza mishipa ya kuchuja damu, kupandikiza figo

 

Hospitali ya Taifa Muhimbili Mloganzila inaendelea na kambi maalum ya ubingwa bobezi ya kutengeneza na kurekebisha mishipa ya kuchuja damu kwa wagonjwa wenye changamoto ya figo, kambi ambayo inaenda sambamba na upandikizaji wa figo kwa wagonjwa wenye changamoto hizo.

Kwa mujibu wa Daktari Bingwa wa Upasuaji Dkt. Daudi Katwana, kambi hiyo inafanywa na wataalam wa hospitali hiyo kwa kushirikiana na jopo la wataalam kutoka Korea Kusini linaloongozwa na Daktari Bingwa Mbobezi wa Upasuaji Dkt. Park Kwan Tae chini ya uratibu wa Taasisi ya Africa Future Foundation (AFF) ya nchini Korea.

“Tulianza kambi hii siku ya Jumamosi Oktoba 11, 2025, ambapo mpaka sasa tumefanikiwa kutengeneza na kurekebisha mishipa ya kuchuja damu kwa wagonjwa wapatao 10, zoezi limeenda vizuri na tutaendelea hadi siku ya Jumanne Oktoba 14, 2025” ameongeza Dkt. Katwana.

Dkt. Katwana amebainisha kuwa huduma hizo ni endelevu, na wapo tayari kuendelea kuhudumia wagonjwa watakaojitokeza hata baada ya kambi hiyo kuisha, hivyo wasisite kufika katika hospitali hiyo ili kunufaika na huduma hizo.

Hospitali ya Taifa Muhimbili Mloganzila ndio hospitali pekee hapa nchini inayotoa matibabu ya ubingwa bobezi ya kupandikiza figo kwa kuvuna figo kutoka kwa mchangiaji kwa kutumia matundu madogo (Hand Assisted Laparoscopic Donor Nephrectomy) huduma ambayo hupunguza muda wa mchangiaji kukaa hospitalini, kutokuwa na makovu makubwa na kupona haraka.

Chapisha Maoni

0 Maoni