BoT yakanusha madai ya kuchapisha fedha kwa ajili ya uchaguzi

 

Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imekanusha taarifa zinazosambaa kwenye mitandao ya kijamii zikidai kuwa taasisi hiyo imechapisha fedha na kuzisambaza kwa ajili ya kugharamia uchaguzi mkuu, ikibainisha kuwa madai hayo hayana ukweli wowote bali ni upotoshaji unaolenga kupotosha umma.

Katika taarifa kwa umma iliyotolewa leo Ijumaa, Oktoba 17, 2025 na kusainiwa na Gavana wa BoT, Emmanuel Tutuba, benki hiyo imesema kuwa baadhi ya wananchi wamekuwa wakihamasishwa kuondoa fedha zao kwenye benki za biashara kwa madai kuwa zinaishiwa fedha kutokana na uchaguzi.

Hata hivyo, BoT imesisitiza kuwa taarifa hizo ni za uongo na zinapaswa kupuuzwa.

“Ninapenda kuwafahamisha wananchi wote kuwa taarifa hizo si za kweli, zinapaswa kupuuzwa na kukemewa wote wanaozisambaza,” imesema BoT.

BoT imefafanua kuwa, kama ilivyo katika nchi nyingine duniani, uchapishaji wa fedha hufanywa kwa mujibu wa sheria. Kwa mujibu wa kifungu cha 26 cha Sheria ya Benki Kuu, Sura ya 197, taasisi hiyo ina jukumu la kuzungusha kiasi cha fedha kinachohitajika katika shughuli za kiuchumi pamoja na mahitaji ya kubadilisha fedha zilizochakaa.

Aidha, benki hiyo imeeleza kuwa fedha huingizwa kwenye mzunguko kupitia benki za biashara na si vinginevyo, na kwamba mchakato huo hufanyika kwa kufuata taratibu rasmi ili kuhakikisha sera za fedha na utulivu wa bei unadhibitiwa ipasavyo.

Chapisha Maoni

0 Maoni