BMH kuanzisha huduma ya kumuondolea mja mzito maumivu wakati wa kujifungua

 

Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) inatarajia kuanzisha huduma mpya ya kumuondolea mama mja mzito maumivu wakati akijifungua kupitia njia ya huduma ya usingizi na ganzi salama kitaalamu inaitwa Epidural anaesthesia.

Hayo yamesemwa na Mtaalamu wa matibabu ya usingizi na ganzi salama wa BMH Fredrick John wakati akitoa mafunzo kwa Watumishi wa Afya na Elimu kwa Wateja wa BMH kama sehemu ya kuadhimisha siku ya usingizi na ganzi salama Duniani.

"Imeonekana baadhi ya wanawake wajawazito wanaogopa yale maumivu ya uchungu  wakati wa kujifungua hivyo wanaomba kujifungua kwa upasuaji, sasa huduma hii tunayoianzisha itamuwezesha mama mja mzito ajifungue  kwa njia ya kawaida bila kusikia maumivu na sio kujifungua kwa upasuaji," alielezea Fredrick.

Huduma hiyo itatolewa kwa ushirikiano wa Wataalamu wa usingizi na ganzi salama, Madaktari wa Magonjwa ya wakina mama na Wauguzi Wakunga na kuwa tayari maandalizi ya vifaa, wataalamu na miongozo viko kwenye hatua nzuri na huduma itaanza kutolewa mwezi Januari 2026.

Nae Mkuu wa Idara ya huduma za usingizi na ganzi salama Dkt. John Venancy Misago amesema kuwa huduma hiyo itakwenda sambamba na kuanzisha matibabu ya maumivu kwa kutumia utaalamu wa usingizi na ganzi salama badala ya dawa ya vidonge vya maumivu (Intervention Pain Management).

"Matibabu hayo ya kitaalamu yatasaidia Wagonjwa wenye Maumivu ya muda mrefu, wenye magonjwa mengine kama ya kansa na wanapata maumivu na Wagonjwa waliotibiwa kwa kufanyiwa upasuaji," aliongezea Dkt. Misago.

Ameongezea kuwa idara yake itatoa mafunzo kwa watoa huduma wa BMH na kisha itaanza programu ya kuzijengea uwezo hospitali nyingine na kuanzisha timu ya Wataalamu wa kuwafuatilia Wagonjwa wa maumivu.

Kaimu Mkurugenzi wa BMH Dkt. Henry Humba pamoja na kuwapongeza Wataalamu hao wa usingizi na ganzi amewataka wasiishie hapo bali kujiendeleza kwa ngazi za juu zaidi  kwa kutambua Hospitali ya Benjamin Mkapa inaendelea kukua, inaendelea kubuni na kuwekeza huduma mpya nyingi ambazo zitahitaji kutumia.

Na. Jeremia Mwakyoma

Picha: Na. Jeremia Mbwambo

Chapisha Maoni

0 Maoni