Waziri Kombo kufanya ziara nchini Uingereza

 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mheshimiwa Balozi Mahmoud Thabit Kombo (MB) kufanya ziara rasmi nchini Uingereza kuanzia tarehe 08 hadi 12 Septemba 2025, inayolenga kuendeleza na kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na wa muda mrefu baina ya Tanzania na Uingereza.

Wakati wa ziara hiyo, Mheshimiwa Waziri Kombo pamoja na mambo mengine, atakuwa Mgeni Rasmi kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika uzinduzi wa kituo kipya cha Taasisi ya ODI Global inayojihusisha kufanya tafiti kuhusu maendeleo utakaofanyika Westminster, London Septemba 09, 2025.

Katika ziara hiyo ambayo inaelezwa inafanyika baada ya takribani miaka 14 tangu Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania alipofanya ziara mara ya mwisho nchini Uingereza. Katika ziara hiyo Mhe. Waziri Kombo pia atakutana na kufanya mazungumzo ya ngazi ya juu na viongozi waandamizi wa Serikali ya Uingereza, Jumuiya za kimataifa, Taasisi za Kifedha, wawakilishi wa kampuni za uwekezaji na wafanyabiashara kwa lengo la kuhamasisha na kutangaza uwekezaji, biashara na utalii nchini Tanzania.

Viongozi wa Serikali na taasisi za kimataifa ambao Waziri Kombo atakutana nao ni pamoja na Mheshimiwa Lord Collins wa Highbury, Waziri wa Uingereza anayeshughulikia masuala ya Afrika; Mheshimiwa Kerry McCarthy (MB), Waziri wa Uingereza anayeshughulia Masuala ya Tabianchi; Mheshimiwa Shirley Ayorkor Botchwey, Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola; na Mheshimiwa Arsenio Dominguez, Katibu Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Bahari (IMO).

Taasisi za kifedha na uwekezaji ambazo Waziri Kombo atakutana na viongozi wake ni pamoja na British International Investment (BII), UK Export Finance (UKEF), King’s Foundation na kushiriki katika meza ya majadiliano ya kibiashara na kampuni teule za Uingereza ili kutangaza fursa za biashara, uwekezaji, nishati safi, miundombinu, na sekta nyingine za kipaumbele zinazopatikana nchini.

Ziara hiyo inatarajiwa kufungua ukurasa mpya wa ushirikiano wa muda mrefu kati ya Tanzania na Uingereza kwa kufungua fursa mpya katika biashara, uwekezaji, mabadiliko ya tabianchi, ubunifu pamoja na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa ndani ya Jumuiya ya Madola.

Imetolewa na: Kitengo cha Mawasiliano Serikalini

Chapisha Maoni

0 Maoni