Umoja wa Mataifa wa Sayansi ya Jiolojia watambua kreta ya Ngorongoro kwa uhifadhi mahiri

 

Umoja wa Mataifa wa Sayansi ya Jiolojia (IUGS) kwa kushirikiana na Mtandao wa jiopaki duniani (GGN) umetambua maeneo ya Jiopaki yanayofanya vizuri katika uhifadhi ambapo eneo la hifadhi ya Ngorongoro kupitia Kreta ya Ngorongoro ni moja la eneo lililotambuliwa kwa uhifadhi wa wanyamapori, mifumo ya ikolojia na uthibiti wa mimea vamizi hali inayofanya eneo hilo kuwa salama.

Utambuzi wa maeneo hayo umetangazwa katika mkutano wa 11 wa kimataifa wa Hifadhi za Jiolojia za UNESCO unaofanyika Mji wa Araucania nchini Chile kuanzia tarehe 8-12 Septemba, 2025 ambao mkutano huo umezikutanisha jiopaki zote duniani Ngorongoro ikiwa ni sehemu ya mkutano huo.

Tanzania kupitia Hifadhi ya Ngorongoro imeshiriki mkutano huu kwa lengo la kubadilishana uzoefu katika kusimamia na kuendeleza Hifadhi ya Jiolojia ya Ngorongoro Lengai ambayo ni jiopaki pekee iliyopo kusini mwa Jangwa la Sahara na ya pili barani Afrika ikitanguliwa na Jiopaki ya M’Goun ya nchini Morocco.

Katika Mkutano huo Hifadhi ya Ngorongoro imewakilishwa na Afisa Uhifadhi Mkuu na mtaalam wa urithi wa Utamaduni Dkt. Agnes Gidna aliyetoa maada ya uzoefu wa kusimamia na kuendesha Jiopaki ya Ngorongoro Lengai pamoja na Afisa Uhifadhi kutoka idara ya Maendeleo ya Jamii Lightness Kiyambile aliyewasilisha mada kuhusu ushiriki wa Jamii na namna wanavyonufaika na uwepo wa Jiopaki ya Ngorongoro.

Eneo la hifadhi ya Ngorongoro lilitambuliwa na UNESCO na kupewa hadhi ya kuwa  Geopark mwaka 2018 ambapo katika mkutano huo NCAA imepata fursa ya kuhamasisha nchi nyingine kufuata nyayo zake katika uanzishaji wa hifadhi za jiolojia, ikiendelea kuwa mfano wa kuigwa na kinara wa uhifadhi endelevu barani Afrika.



               
                     Na. Mwandishi Wetu - Chile

Chapisha Maoni

0 Maoni