Samia: Tumejipanga kuboresha barabara, reli na bandari kavu Tunduma

 

Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mhe. Samia Suluhu Hassan, ameahidi kuimarisha sekta ya miundombinu nchini ikiwa ni pamoja na barabara, reli na bandari kavu, ili kuongeza ufanisi wa usafirishaji na kuimarisha biashara kati ya Tanzania na nchi jirani.

Akizungumza leo Jumatano, Septemba 3, 2025, katika mkutano wa kampeni uliofanyika eneo la Tunduma Mpakani, wilayani Momba mkoani Songwe, Mhe. Samia alisema kuwa Serikali tayari imeanza kuchukua hatua za awali za kuboresha barabara na reli zinazounganisha Tanzania na Zambia, ikiwa ni sehemu ya ajenda pana ya kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha usafirishaji na biashara ukanda wa Kusini mwa Afrika.

“Tumeanza kazi ya maboresho ya miundombinu muhimu, na tunaendelea kuifanyia kazi reli ya Tazara kwa ukarabati wa kiwango cha juu ili kuongeza kasi ya usafirishaji wa mizigo. Tayari tumeshatia saini makubaliano na Serikali ya China kufanikisha mradi huu muhimu,” alisema Samia mbele ya maelfu ya wananchi waliojitokeza kwenye mkutano huo.

Bandari kavu Mpemba kuondoa msongamano

Katika hatua nyingine, Samia alieleza kuwa Serikali itakamilisha ujenzi wa bandari kavu (dry port) katika Kata ya Mpemba, Tunduma, yenye ukubwa wa ekari 1,800, ambayo inalenga kupunguza msongamano wa malori na kurahisisha shughuli za usafirishaji mipakani.

“Bandari hii kavu itarahisisha biashara kati ya Tanzania na Zambia, pamoja na kupunguza muda wa kusafirisha mizigo. Hii ni sehemu ya mkakati wetu wa kuifanya Tunduma kuwa lango la kimkakati la kiuchumi,” alisema.

Samia pia alitumia nafasi hiyo kuwasihi wananchi wa mkoa wa Songwe na maeneo ya mpakani kushiriki kikamilifu katika zoezi la uchaguzi kwa amani, huku akisisitiza kuwa Serikali ya CCM itaendelea kujenga miundombinu bora inayogusa maisha ya wananchi wa kawaida.


Chapisha Maoni

0 Maoni