Kamati ya Mawasiliano Wizara ya Fedha yahimizwa kuboresha utoaji taarifa

 

Mwenyekiti wa Kamati ya Mawasiliano ambaye pia ni Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini katika Wizara ya Fedha, Bw. Benny Mwaipaja, amewataka wajumbe wa kamati hiyo kuhakikisha wanashiriki kikamilifu katika kutoa taarifa sahihi na kwa wakati kwa umma, ili kusaidia utekelezaji wa haki ya wananchi ya kupata taarifa.

Akizungumza jijini Dodoma wakati wa kikao kazi cha Kamati hiyo, kilichowakutanisha wajumbe kutoka idara na vitengo mbalimbali vya wizara hiyo, Bw. Mwaipaja alisema lengo kuu ni kurahisisha upatikanaji wa taarifa kwa matumizi ya umma.

"Wizara ina jukumu la msingi la kuwapatia wananchi taarifa kuhusu sera, mipango, programu na matukio mbalimbali ya kisekta, ili kuwawezesha kuelewa majukumu ya wizara na mchango wake katika maendeleo ya nchi," alisema Bw. Mwaipaja.

Aliongeza kuwa wajumbe wa kamati hiyo wanapaswa kutoa ushirikiano wa karibu kwa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini kwa kuwasilisha kalenda za matukio muhimu mapema, ili kurahisisha uratibu na upashanaji taarifa kwa njia mbalimbali.

"Napenda kusisitiza kuwa taarifa mnazozitoa si tu kwamba zinasaidia kuandaa majarida ya wizara, bali pia hutumika kwenye tovuti ya wizara, mitandao ya kijamii kama Instagram, WhatsApp, Twitter, LinkedIn, Hazina TV na hata kwenye vyombo vya habari vya kitaifa kama runinga na magazeti," alisema.

Aidha, alieleza kuwa tayari wizara imetoa toleo la nne la Jarida la Hazina Yetu, ambalo linasheheni taarifa mbalimbali muhimu kwa wananchi, huku maandalizi ya toleo la tano yakiwa yanaendelea, yakitegemea taarifa kutoka katika idara na vitengo vya wizara.

Bw. Mwaipaja alisema kuwa kupitia matumizi ya lugha nyepesi na yenye kueleweka, majarida hayo yamekuwa yakipokelewa vyema na wadau mbalimbali wa ndani na nje ya wizara, ambao sasa wameonyesha nia ya kuendelea kushiriki kikamilifu katika mchakato wa upatikanaji na usambazaji wa taarifa.

Katika hatua nyingine, aliwataka wajumbe hao kuendelea kuhamasisha wadau mbalimbali kufuatilia taarifa rasmi zinazotolewa na wizara, kwa ajili ya kuongeza maarifa, kufanya tafiti za kitaaluma na matumizi mengine yenye tija kwa jamii.




Chapisha Maoni

0 Maoni