Wizara ya Afya Zanzibar kuimarisha ushirikiano na taasisi ya The Same Qualities Foundation

 


Wizara ya Afya Zanzibar imesema itaendelea kuimarisha ushirikiano wake na Taasisi ya The Same Qualities Foundation kutoka Arusha, kwa lengo la kuboresha huduma za afya kwa wananchi wa Zanzibar, hususan matibabu ya watoto na watu wazima wenye tatizo la midomo wazi.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Afya Zanzibar, Nassor Ahmed Mazrui, alipofanya ziara maalum katika kambi ya matibabu ya midomo wazi inayoendelea kufanyika katika Hospitali ya Mkoa Lumumba. Kambi hiyo inaendeshwa kwa ushirikiano kati ya madaktari bingwa kutoka taasisi hiyo ya Arusha na wataalamu wa ndani kutoka Zanzibar.

“Matibabu yanayotolewa katika kambi hii ni bure kabisa na dawa zipo za kutosha. Naomba niwasihi wazazi wenye watoto wenye matatizo haya wawatoe majumbani, wawafikishe hospitalini ili wapatiwe huduma. Wakitibiwa vizuri, wanarejea katika hali ya kawaida na kupata heshima yao katika jamii,” alisema Waziri Mazrui.

Amesema kuwa, kwa kuunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Afya, taasisi hiyo imekuwa ikileta mara mbili kwa mwaka madaktari bingwa kutoka mataifa mbalimbali kutoa huduma hizo bure kwa wananchi wa Unguja na Pemba.

“Tumeshuhudia wagonjwa waliopata huduma hizi katika awamu zilizopita, wengi wao wanaendelea vizuri kiafya. Tunaamini hata safari hii huduma zitatolewa kwa ufanisi mkubwa,” aliongeza Waziri Mazrui.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa waandaaji wa kambi hiyo, huduma hizo za upasuaji na tiba za midomo wazi zimeanza kutolewa rasmi tangu Jumatatu, Agosti 25, na zitahitimishwa Ijumaa, Agosti 29, ambapo jumla ya watu 25 wanatarajiwa kupatiwa matibabu.

The Same Qualities Foundation ni miongoni mwa taasisi zinazotoa mchango mkubwa katika sekta ya afya Tanzania Bara na Zanzibar, kwa kutoa huduma za kibingwa kwa watu wenye matatizo ya kinywa na uso, hasa midomo wazi, bila malipo.



Chapisha Maoni

0 Maoni