Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii kuraisisha Huduma za Afya Zanzibar

 

Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi, Idrisa Kitwana Mustafa, amesema kuwa utambulisho wa Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii (CHW) ni hatua muhimu inayochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa lengo la kurahisisha utoaji wa huduma za afya na kupunguza vifo na magonjwa ya kina mama na watoto kwa wananchi wa Zanzibar.

Mkuu huyo wa Mkoa ameyasema hayo katika hafla ya utambulisho na makabidhiano ya Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii kutoka Wizara ya Afya Zanzibar kwenda Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi, iliyofanyika katika Ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdul Wakil, Kikwajuni  Zanzibar.

Amesema kuwa wahudumu hao ni nguzo muhimu katika mapambano dhidi ya maradhi mbalimbali na kuimarisha afya ya mama na mtoto. Aidha, ameeleza kuwa dhamira ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ni kuwapandisha hadhi wahudumu hao kutoka kujitolea (CHV) hadi kuwa wafanyakazi rasmi, ili wawe sehemu ya juhudi za Serikali katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya kuanzia ngazi ya jamii hadi hospitali za rufaa.

Amewahimiza Wahudumu hao kufanya kazi kwa weledi, uadilifu na bidii, wakishirikiana na viongozi wa serikali za mitaa na mikoa ili kufanikisha azma ya Serikali ya kuimarisha afya ya jamii. Pia amewataka kuwa waadilifu katika utendaji wao na kuwa tayari kushirikiana kwa karibu na wananchi kwa lengo la kujenga jamii yenye afya bora.

Viongozi wa Wizara ya Afya wamepongezwa kwa mchango wao katika kuwaendeleza wahudumu hao na kusimamia mchakato wa kuwatambua rasmi na kuwakabidhi kwa viongozi wa mkoa na serikali za mitaa, hatua itakayochochea maendeleo ya huduma za afya nchini.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Afya Zanzibar, Hassan Khamis Hafidh, amesema nchi nyingi zilizoendelea zimefanikiwa katika huduma za afya kupitia mfumo wa kinga unaotegemea wahudumu wa afya wa ngazi ya jamii. Hivyo ni wakati muafaka kwa CHW kubeba jukumu hilo kama nguzo ya kwanza ya uimarishaji wa huduma bora za afya kwa jamii.

Ameeleza kuwa jukumu jingine la CHW ni kuimarisha uelewa wa afya katika jamii kwa kila kaya, shehia na wilaya, sambamba na kutoa elimu ya kinga pamoja na uchunguzi wa awali na rufaa pale inapohitajika.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt. Amour Suleiman Mohammed, amesema mpango wa kuwatambua CHW ni utekelezaji wa ahadi ya Rais Dkt. Mwinyi. Hadi sasa jumla ya CHW 651 katika Mkoa wa Mjini Magharibi wamehitimu mafunzo ya miezi sita na tayari wameanza kazi za kijamii.

Amefafanua kuwa CHW sasa watakuwa chini ya usimamizi wa viongozi wa mikoa na wilaya, wakijikita zaidi katika kutoa elimu ya afya, kushiriki katika kampeni za jamii, kupinga ukatili wa kijinsia, kushiriki tafiti za afya na kusaidia kupunguza vifo na kuimarisha utoaji wa huduma bora za afya.

Mkurugenzi wa Kinga na Elimu ya Afya Zanzibar, Dkt. Salim Slim, amesema uwepo wa CHW katika jamii ni nyenzo muhimu ya kusaidia Serikali kupunguza rufaa zisizo za lazima kwa wagonjwa kwenda hospitali kubwa kwa kuwa huduma za kinga zitapatikana mapema. Ameahidi kuwa Wizara itaendelea kushirikiana nao ili kufanikisha malengo ya sekta ya afya.

Mratibu wa Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii, Halima Ali Khamis, amesema hadi sasa jumla ya CHW 1,242 wamekamilisha mafunzo yao, huku wengine 1,054 wakiendelea na mafunzo, ikiwa ni sehemu ya uimarishaji wa upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi katika maeneo yao.

Wawakilishi kutoka mashirika ya kimataifa ya WILLOSA na D-Tree, Abdul-Wahid Habib na Anna Mikidadi, wamesema CHW ni kiunganishi muhimu kati ya familia na vituo vya afya. Wamehimiza ushirikiano baina ya serikali na wadau wengine katika kuhakikisha huduma bora za afya ya mama na mtoto zinaimarika, huku wakiahidi kuendeleza matunda ya kazi chanya kwa jamii.

Kwa sasa, Mkoa wa Mjini Magharibi una jumla ya CHW 651 waliomaliza mafunzo na tayari wameanza kazi. Katika Wilaya ya Mjini, CHW 201 wamehitimu na kuanza kazi ambapo idadi kamili itakapokamilika itafikia 404. Wilaya ya Magharibi “A” ina CHW 239 waliomaliza mafunzo, na idadi hiyo ikikamilika itafikia 549. Wilaya ya Magharibi “B” ina CHW 211 waliomaliza mafunzo na kuanza kazi rasmi; na idadi kamili itafikia 634 baada ya mafunzo kukamilika.

Makabidhiano haya yaliambatana na kiapo cha utendaji kazi kilichotolewa kwa CHW na Naibu Waziri wa Afya Zanzibar Hassan Khamis Hafidh.




Chapisha Maoni

0 Maoni