TCRA yawafunda Mabloga kuelekea Uchaguzi Mkuu 2025

 

Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imewataka waandishi wa habari kutokuwa sehemu ya kukuza migogoro katika kipindi cha uchaguzi mkuu na kuwaasa wajiulize kwanza habari wanayotaka kuitoa iwapo italeta athari gani kwa jamii na kwa amani ya nchi.

Hayo yameelezwa leo Jijini Dar es Salaam na Meneja Kitengo cha Huduma za Utangazaji TCRA, Mhandisi Andrew Kisaka katika mafunzo yaliyotolewa kwa Mtandao wa Wana Blogu wa Tanzania (TBN) ambapo mada saba ziliwasilisha ili kuwajengea uwezo mabloga kuelekea uchaguzi mkuu.

“Katika machafuko na migogoro waandishi wa habari mnapaswa kuangalia taarifa zenu mnazochapisha na kuzitangaza ili msiwe sehemu ya kukuza migogoro na kuhatarisha amani na utulivu,” alisema Mhandisi Kisaka.

Mhandisi Kisaka amewahimiza waandishi wa habari kuzingatia kutoa elimu kwa mpiga kura, kutoa taarifa za mwenendo wa kampeni, kutoa taaria ya nini kinaendelea wakati wa uchaguzi pamoja na kutangaza matokeo yatakayotolewa na Tume Huru ya Uchaguzi (INEC).

Kwa upande wao Wahadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Dkt. Engbert Mkoko na Dkt. Darius Mukiza wakitoa mada kwa nyakati tofauti walisisiti waandishi wa habari kuzingatia sheria mbalimbali wakati wakitekeleza majukumu yao katika kipindi chote cha uchaguzi na kuwa makini na habari za upotoshaji.

Naye Afisa kutoka Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari-JAB, Rehema Mpagama akiongea kwa niaba ya Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula amewataka waandishi wa habari kuhakikisha kuwa wamepatiwa kwanza ithibati na kupewa press card ndipo washiriki kuripoti uchaguzi mkuu.

Kwa upande wake Mkuu wa Uhusiano na Mawasiliano - PDPC, Innocent Mungy amewatahadharisha waandishi wa habari kuwa katika kipindi hiki cha uchaguzi kuna vihatarishi vingi vinavyohusiana ukiukaji wa ulinzi wa taarifa binafsi.

Awali Kaimu Mwenyekiti wa TBN, Beda Msimbe alitoa shukrani kwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Katibu Mkuu wake, Ndugu Gerson Msigwa, kwa kuona umuhimu wa TBN na kuwezesha mafunzo hayo.

Pia, aliishukuru Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kwa kuandaa na kuratibu mafunzo haya muhimu ambayo yanalenga kutuandaa mabloga kuripoti habari za uchaguzi kwa weledi na uadilifu.

Beda amesema kuwa kwa miaka mingi, Mtandao wa Mabloga Tanzania (TBN) umekuwa sauti muhimu katika jamii. “Tumekuwa jukwaa huru linalowapa Watanzania fursa ya kutoa mawazo yao, kushiriki uzoefu, na kujadili masuala mbalimbali yanayohusu jamii yetu.”

“Jukumu letu si tu kutoa habari, bali pia kuhakikisha habari hizo ni sahihi na zinazingatia maadili na utamaduni wa Kitanzania. Tunapaswa kulaani vikali wale wote wanaokwenda kinyume na maadili yetu, wanaosambaza habari za uongo na za uchochezi,” alisema Beda.

Chapisha Maoni

0 Maoni