Tanzania, Sweden zaimarisha ushirikiano wa kidiplomasia na kiuchumi

 

Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Mhe. Mobhare Matinyi, leo Agosti 22, 2025, amekutana na kufanya mazungumzo rasmi na Waziri wa Mambo ya Nje wa Sweden, Mhe. Maria Malmer Stenergard, katika ofisi za wizara hiyo jijini Stockholm, ikiwa ni sehemu ya kuendeleza uhusiano wa muda mrefu kati ya mataifa hayo mawili.

Katika mazungumzo hayo, Mhe. Balozi Matinyi aliwasilisha salamu kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye alimtaja kama Mwanadiplomasia namba moja wa taifa, huku akisisitiza dhamira ya Tanzania kuimarisha mahusiano ya kidiplomasia na kukuza ushirikiano wa kiuchumi na Sweden.

Balozi Matinyi alieleza kuwa Tanzania imeendelea kuweka kipaumbele kwenye ushirikiano wa kimataifa, hasa katika sekta za nishati, elimu, afya, utafiti, mazingira, viwanda na miundombinu ikiwemo ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR).

“Tanzania inatambua mchango mkubwa wa Sweden katika kusaidia maendeleo ya sekta mbalimbali na tunaamini ushirikiano huu utaendelea kuleta manufaa kwa pande zote mbili,” alisema Mhe. Matinyi.

Aidha, alibainisha kuwa hadi sasa jumla ya kampuni 101 kutoka Sweden zimewekeza nchini Tanzania katika sekta mbalimbali, kwa thamani ya zaidi ya dola za Marekani milioni 313.04, huku zikiwa zimezalisha ajira takribani 3,877. Alisisitiza kuwa Tanzania inakaribisha kwa mikono miwili wawekezaji kutoka Sweden ili kuendeleza biashara na miradi ya pamoja.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje wa Sweden, Mhe. Stenergard, alieleza kuwa Sweden inaendelea kuthamini ushirikiano wake na Tanzania, na iko tayari kupanua wigo wa mahusiano hayo, hasa kwenye biashara na uwekezaji.

Vilevile, Waziri Stenergard alitoa pongezi kwa Tanzania kwa mchango wake katika kulinda amani na usalama wa kimataifa, huku akihimiza ushiriki wa Tanzania katika kutafuta suluhisho la kudumu la mgogoro kati ya Ukraine na Urusi.

Mazungumzo hayo ni sehemu ya juhudi za kidiplomasia zinazolenga kuimarisha nafasi ya Tanzania katika jukwaa la kimataifa, pamoja na kuhamasisha uwekezaji unaolenga maendeleo endelevu.

Chapisha Maoni

0 Maoni