INEC yawataka Wazalisha wa Maudhui Mtandaoni kuandika habari za kweli

 

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mheshimiwa Jaji wa Mahakama ya Rufaa Jacobs Mwambegele, amewataka wazalishaji wa maudhui mtandaoni kuhakikisha kuwa taarifa  za uchaguzi wanazoziweka kwenye kurasa zao za mitandao ni za kweli na zisizokuwa na chembe ya upotoshaji.

Akizungumza leo Agosti 3, 2025 wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Kitaifa baina ya INEC na Wazalishaji wa Maudhui Mtandaoni, Jaji Mwambegele ameeleza kwamba ukosefu wa umakini katika utoaji wa habari wakati uchaguzi mkuu unaweza kuharibu na kuhatarisha amani na utulivu wa nchi.

“Ni ukweli kwamba mitandao hasa ya kijamii imekuwa ni chanzo muhimu cha habari kutokana na kuwa taarifa zinazochakatwa kwenye mitandao zinapatikana kwa urahisi na kwa haraka hiyo basi ni muhimu kuhakikisha habari hizo zinakuwa ni za kweli,” amesema Jaji Mwambegele.

Jaji Mwambegela pia, amewaasa Wazalishaji wa Maudhui  Mtandaoni kuepuka matumizi mabaya ya Akili Unde (AI) ambayo inatumiwa na baadhi ya watu wenye nia ovu kusambaza habari za upotoshaji kupitia mitandao ya kijamii.

Kuhusiana na madai ya kuwa idadi ya wapiga kura walioandikishwa kwenye daftari la kudumu la kupiga kura inawezekana kuwa si sahihi kutokana na uwezekano wa kuwapo watu waliokufa kwenye daftari hilo Jaji Mwambegele amesema;

“Nikweli huenda kukawa na watu waliokufa kwenye daftari la wapiga kura iwapo hatujapata taarifa za mpiga kura aliyepoteza maisha lakini tukipata taarifa hiyo tutamuondoa, ila hata hivyo hakuna mtu aliyekufa anaweza kupiga kura hivyo uwepo wao unajaza nafasi tu hauathiri upigaji kura,” alisema Jaji Mwambegele.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Uchaguzi Kailima Ramadhani amesema tume imejiwekea utaratibu wa kuvishirikisha vyombo vya habari katika mchakati mzima wa uendeshaji uchaguzi ili kuweka uwazi na kuhakikisha wanashiriki kikamilifu.

“Tunatarajia kupata ushirikiano kutoka kwenu ili kuhakikisha kuwa uchaguzi mkuu unafanyika kwa amani na utulivu, na iwapo kutakuwa na changamoto, fuateni Sheria, Kanuni, Miongozo, Taratibu na Maelekezo mbalimbali yaliyotolewa na yatakayotolewa na INEC,” amesema Ramadhani.




Chapisha Maoni

0 Maoni