Zaidi ya wananchi 45,000 watembelea banda la Maliasili na Utalii Sabasaba

 

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Mej.Jen (Mstaafu) Hamis Semfuko amesema kuna mwitikio mkubwa sana wa wananchi kutembelea banda la Wizara ya Maliasili na Utalii na takribani watalii zaidi ya 45,000 walitembelea banda hilo kwa siku ya jana Julai 5,2025.

Mej. Jen (Mstaafu) Semfuko ameyasema hayo leo Julai 6,2025 alipotembelea Bustani ya Wanyamapori katika Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara yanayoendelea katika viwanja vya Sabasaba akiambatana na Menejementi ya TAWA.

“Nimefurahi sana kuona mwitikio mkubwa wa wananchi kutembelea banda la Wizara yetu hususan katika Bustani ya Wanyamapori na hapa nimejulishwa kuwa kwa siku ya jana pekee takribani wananchi 45,000 walitembelea banda la Wizara ya Maliasili na Utalii,” amesema Semfuko.

Mej. Jen (Mstaafu) Semfuko ameongeza kuwa mwitikio huu wa wananchi umechagizwa na sababu mbalimbali zikiwemo jitihada zilizofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt Samia Suluhu Hassan katika kutangaza vivutio vya utalii nchini.

“Tunamshukuru Mhe. Rais kwa  jitihada alizofanya za kutangaza utalii zimesababisha watu wapende kuona wanyamapori na vivutio vingine vya utalii,” ameongeza Semfuko.

Sambamba na hilo, Semfuko amesema kuwa hivi karibuni TAWA imejipanga kuanzisha Bustani ya Wanyamapori katika Visiwa vya Zanzibari katika Hifadhi ya Jambiani Muyuni.

“Hivi karibuni TAWA tutapeleka mbawa zetu Zanzibar, ukifika Zanzibar, ukaenda Jambiani utatukuta TAWA pale, hivyo karibuni sana,” amesema Semfuko.

Kwa upande wake, Kaimu Kamishna wa Uhifadhi TAWA, Mlage Kabange amesema TAWA imendelea kuleta wanyamapori katika maonesho haya kwa lengo la kuwapa elimu  wananchi kuhusu wanyamapori hao sambamba na kuhamasisha wananchi kutembelea vivutio vya utalii.

Kadhalika, Kamishna Kabange amesema wanashukuru kuona mwitikio mkubwa wa watu katika kuona wanyamapori, Aidha, amesema kuwa baada ya maonesho ya Sabasaba kukamilika wanyamapori hawa wataendelea kupatikana katika Hifadhi ya Pande iliyoko jijini Dar es Salaam.

“Baada ya maonesho haya kumalizika, wanyamapori hawa bado wataendelea kuwepo katika maeneo mbalimbali tunayoyasimamia, kwa Dar es Salaam tuna eneo la Pande na wanyama hawa wote waliopo hapa, wanapatikana kule hivyo tunawakaribisha wananchi baada ya Sabasaba waendelee kutembelea maeneo tunayosimamia,” amesema Kamishna Kabange.

Maonesho ya Sabasaba bado yanaendelea katika viwanja vya Sabasaba hadi ifikapo 13 Julai 2025. 



                        Na. Joyce Ndunguru - Dar es Salaam

Chapisha Maoni

0 Maoni