Waziri Gwajima atoa pole vifo vya watoto 5 Tabora

 

Serikali kupitia Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum imepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya vifo vya watoto watano waliopoteza maisha katika ajali ya moto iliyotokea usiku wa Julai 28, 2025 katika Makao ya Watoto ya Igambilo, Manispaa ya Tabora.

Katika taarifa iliyotolewa jana na Waziri wa wizara hiyo, Dkt. Dorothy Gwajima, Serikali imetoa pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki walioguswa na msiba huo mzito, huku ikitoa wito kwa jamii kuwaombea waliopoteza wapendwa wao faraja, subira na nguvu katika kipindi hiki kigumu.

"Tunasikitika kwa msiba huu mkubwa uliogharimu maisha ya watoto wetu. Tunaungana na familia zao na wote walioguswa katika maombi na pole nyingi," amesema Dkt. Gwajima.

Waziri huyo pia ameliagiza Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi wa kina kubaini chanzo cha ajali hiyo ya moto, na kuhakikisha hatua stahiki zinachukuliwa kwa mujibu wa sheria.

Aidha, Dkt. Gwajima ametoa wito kwa wamiliki na wasimamizi wa Makao yote ya Watoto nchini kufanya ukaguzi wa mara kwa mara wa mifumo ya umeme, sambamba na kuweka miundombinu ya kudhibiti majanga ya moto ili kuzuia ajali za aina hiyo kujirudia.

Serikali imesema tayari imechukua hatua kuhakikisha majeruhi wa tukio hilo wanapata matibabu bure, huku watoto wengine waliokuwepo katika makao hayo wakihamishwa na kupelekwa katika mazingira salama, sambamba na kusaidiwa kisaikolojia na kijamii kupitia Maafisa Ustawi wa Jamii.

"Wizara itaendelea kufuatilia kwa karibu mwenendo wa tukio hili na kuchukua hatua stahiki za kuimarisha ulinzi na usalama wa watoto wote walioko katika Makao ya Watoto nchini," imeeleza taarifa hiyo.

Tukio hilo linaibua maswali juu ya hali ya usalama katika baadhi ya vituo vya kulelea watoto nchini, huku wadau wa haki za watoto wakitaka hatua madhubuti zichukuliwe kuzuia madhara kama haya siku za usoni.

Chapisha Maoni

0 Maoni