Watanzania bara kupiga kura Uchaguzi Mkuu Oktoba 29

 

Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) imetangaza rasmi kuwa Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na Madiwani kwa Tanzania Bara utafanyika Jumatano, tarehe 29 Oktoba, 2025.

Akizungumza leo katika hafla ya uzinduzi wa ratiba ya uchaguzi iliyofanyika makao makuu ya Tume, Njedengwa jijini Dodoma, Mwenyekiti wa INEC, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele amesema jumla ya wapiga kura waliojiandikisha ni 37,655,559, ikiwa ni ongezeko la asilimia 26.55 kutoka wapiga kura 29,754,699 walioandikishwa mwaka 2020.

Ratiba ya Uteuzi na Kampeni

Jaji Mwambegele ameeleza kuwa utoaji wa fomu za uteuzi kwa wagombea wa nafasi ya Rais na Makamu wa Rais utafanyika kuanzia 9 Agosti hadi 27 Agosti, 2025. Kwa wagombea ubunge na udiwani, utoaji wa fomu utaanza 14 Agosti hadi 27 Agosti, 2025.

Tarehe 27 Agosti, 2025, itakuwa ni siku rasmi ya uteuzi wa wagombea kwa nafasi zote; Rais na Makamu wa Rais, Wabunge, na Madiwani.

Kampeni za uchaguzi kwa Tanzania Bara zitaanza 28 Agosti hadi 28 Oktoba, 2025, huku kwa upande wa Tanzania Zanzibar kampeni zitadumu hadi 27 Oktoba, 2025, ili kupisha zoezi la kupiga kura ya mapema.

Katika jumla ya wapiga kura waliojiandikisha

Tanzania Bara inajumuisha 36,650,932, na upande wa Tanzania Zanzibar inajumuisha 1,004,627, ambapo 725,876 wameandikishwa na ZEC na 278,751 wameandikishwa na INEC kwa kuwa hawakuwa na sifa za kuandikishwa na ZEC.

Kuhusu jinsia

Wanawake ni 18,943,455 (asilimia 50.31),

Wanaume ni 18,712,104 (asilimia 49.69),

Watu wenye ulemavu ni 49,174

Vituo vya Kupigia Kura

Jaji Mwambegele amesema jumla ya vituo 99,911 vitatumika katika uchaguzi huu:

97,349 vitakuwa Tanzania Bara, 2,562 vitakuwa Tanzania Zanzibar. Idadi hiyo ni ongezeko la asilimia 22.49 kutoka vituo 81,567 vilivyotumika kwenye uchaguzi wa mwaka 2020.

Wito kwa Wananchi, Mwenyekiti wa INEC ametoa wito kwa wananchi na wadau wote wa uchaguzi kushiriki kikamilifu katika mchakato wa uchaguzi huku wakizingatia sheria, kanuni, miongozo, na maelekezo yatakayotolewa na Tume.

"Ushiriki wa wananchi ni kiini cha mafanikio ya uchaguzi huru na wa haki," amesisitiza Jaji Mwambegele.

Chapisha Maoni

0 Maoni