Rais Samia kuzindua Dira ya Taifa 2050 Julai 17 Dodoma

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuzindua Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 Julai 17, 2025 jijini Dodoma, kufuatia kukamilika kwa mchakato wa dira hiyo ya 2050 ya Tanzania Tuitakayo.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam alipokutana na Jukwaa la Wahariri Tanzania kuelezea kuhusu maandalizi ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 yalipofikia.

“Dira ya Taifa ya 2050 imepitia hatua 13, sasa imeshakamilika rasmi ambapo Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ataizindua rasmi Julai 17, 2025 jijini Dodoma katika ukumbi wa Jakaya Kikwete Convention Centre,” alisema Prof. Mkumbo.

Ameeleza kwamba, katika kuhakikisha kuwa dira hiyo inatekelezwa na awamu zote zitakazokuja hadi kufikia 2050, Rais Samia alimuagiza kuiwasilisha bungeni dira hiyo kwa ajili ya kuidhinishwa na bunge, na alifanya hivyo katika kikao cha mwisho cha bunge lililomaliza muda wake.

“Tumepeleka Dira ya 2050 bungeni ili kuhakikishakuwa hakuna kiongozi atakayeingia madarakani na kuamua kuacha kuitekeleza Dira ya 2050 na kuja na mipango yake mingine…labda arudi tena bungeni kuomba ridhaa ya kufanya mabadiliko,” alisema Prof. Mkumbo.

Ameongeza kuwa pia, wao kama wanasiasa wamekubaliana kuhakikisha kuwa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inatekelezwa kwa kuhakikisha kila chama kinakuwa na Ilani ambayo inaakisi mambo yaliyomo kwenye dira hiyo.

Amesema kuwa dira hiyo imeshirikisha watu wa makundi mbalimbali wapatao milioni 1.2 ambapo katika yao kundi kubwa lilikuwa la vijana, pia waliwafikia viongozi wastaafu na walio madarakani 44 ili kupata mchango wao.

Pamoja na mambo mengine, Prof. Mkumbo amesema kwamba Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 itaanza kutumika Julai mosi 2026, baada ya kumalizika kwa Dira ya sasa June 31, 2026, hivyo serikali inamuda wa kutosha wa kujiandaa kwa utekelezaji wake.





Chapisha Maoni

0 Maoni