Washindwa kuwagharamia wanyama wao kwa ugumu wa maisha Nigeria

 

Mmiliki wa mbwa Preye Maxwell anaonekana mwenye huzuni anapomuacha mbwa wake mpendwa Hanks katika hifadhi ya wanyama katika jijini Lagos ambalo ni kitovu cha biashara cha Nigeria.

Akibubujikwa na machozi, anasema: "Siwezi kumudu kumtunza. Siwezi kumlisha kwa njia anayostahili kulishwa."

Mbwa huyo wa miaka miwili aina ya American Eskimo anabweka wakati mmiliki wake anageuka na kuondoka katika Taasisi ya Uokoaji Wanyama ya St Mark’s iliyoko katika kitongoji cha Ajah, Lagos.

Dkt. Mark Afua, daktari wa wanyama na mwenyekiti wa kituo hicho cha uokoaji, anamchukua Hanks na kumuweka kwenye kizimba cha banda kubwa la chuma, katika moja ya vyumba vingi vya jengo la ghorofa moja lililoundwa kwa ajili ya kuhifadhiwa mbwa, paka, nyoka na wanyama wengine.

Maxwell, mtaalamu wa mikakati ya vyombo vya habari mtandaoni, alipoteza ajira hivi karibuni. Kutafuta kazi kumemfanya asiwepo nyumbani mara nyingi, na hivyo kuhisi hawezi kumtunza Hanks ipasavyo.

Uamuzi wa kijana huyo mwenye umri wa miaka 33 haukuwa rahisi, lakini ni hatua ambayo wamiliki wengi wa wanyama wa nyumbani wanachukua kutokana na kupanda kwa gharama za maisha nchini Nigeria.

Taifa hilo lenye watu wengi zaidi barani Afrika limekumbwa na mfumuko mkubwa wa bei tangu Rais Bola Tinubu aingie madarakani miaka miwili iliyopita na kuondoa ruzuku ya mafuta ambayo ilikuwa ikitumika kwa muda mrefu.

Chapisha Maoni

0 Maoni