Shirika la Nyumba la
Taifa (NHC) limefanikiwa kupata faida ya Shilingi bilioni 235.4 katika kipindi
cha miaka mitano (2018/19 hadi 2023/24), ikiwa ni ongezeko la faida kwa
asilimia 33.1 katika kipindi hicho.
Taarifa hiyo
imetolewa leo jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Bw. Hamad
Abdallah Hamad, wakati wa mkutano na wahariri wa vyombo vya habari
waliotembelea miradi mbalimbali ya shirika hilo ikiwemo Morocco Square, Kawe
711, Golden Premier Resident (GPR) na Samia Scheme Kawe.
Bw. Hamad amesema
katika mwaka wa fedha wa Julai 2023 hadi Juni 2024, NHC imepata faida kabla ya
kodi ya Shilingi bilioni 36.8, ikiwa ni sawa na asilimia 112.5 ya lengo, kwa hesabu
zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).
Aidha, Bw. Hamad
ameongeza kuwa mtaji wa Shirika umeendelea kuimarika, ambapo hadi kufikia Juni
2024 mtaji huo umefikia Shilingi trilioni 5.5, ukilinganishwa na Shilingi trilioni
5.08 mwaka uliopita.
“Katika kipindi cha
miaka mitano (2019/20 hadi 2023/24), NHC imelipa kodi mbalimbali kwa Serikali
zinazofikia jumla ya Shilingi bilioni 134.4, huku gawio kwa Serikali katika
kipindi hicho kikifikia Shilingi bilioni 9.85,” alisema Bw. Hamad.
Kwa mwaka huu wa 2025
pekee, NHC imelipa gawio la Shilingi bilioni 5.5, na kufanikiwa kuweka rekodi
ya kuwa shirika lililoongoza kwa ongezeko la gawio, hatua iliyowezesha kupatiwa
tuzo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.
“Rais Dkt. Samia
alitueleza kuwa anataka kuona NHC inatoa gawio la Shilingi bilioni 10, nasi
tumejipanga kufikia huko na tuna timu nzuri yenye wataalam watakaoweza
kufanikisha hilo,” aliongeza Bw. Hamad.
Kwa upande wa mapato,
Mkurugenzi huyo alisema Shirika hilo limeendelea kuimarika, ambapo mapato
yameongezeka kutoka Shilingi bilioni 125 mwaka 2019/20 hadi Shilingi bilioni
189 mwaka 2023/24, sawa na ongezeko la asilimia 34.
Mapato hayo, kwa
mujibu wa Bw. Hamad, tayari yamekaguliwa rasmi na CAG, jambo linaloonyesha
uwazi na ufanisi wa uendeshaji wa shirika hilo la umma.

0 Maoni