Matunda mazuri ya uvuvi wa vizimba yaanza kuonekana Musoma Vijijini

 

Wavuvi wa Jimbo la Musoma Vijijini Mkoani Mara wameanza kupata matunda mazuri kutokana na uvuvi wa samaki kwa kutumia vizimba, ambao Mbunge wa Jimbo hilo, Prof. Sospeter Muhongo amekuwa mstari wa mbele kuhimiza uvuvi huo katika Ziwa Victoria.

Wakiongea kwa nyakati tofauti mmoja wa wavuvi walionufaika na uvuvi wa samaki kwa kutumia vizimba katika Kijijini Kigera, Kitongoji cha Kurukiri amesema anavuna samaki takribani Tani 40 kutoka kwenye vizimba vyake 4 vyenye upenyo wa mita 10.

Amesema masoko ya samaki wanaovunwa kutoka kwenye vizimba yapo, ambayo ni ya walaji na viwanda vya minofu ya samaki. “Bei inaendana na ukubwa na uzito wa samaki, na kwa sasa ni kati ya Shilingi 7,000 na 10,000 kwa kilo moja.”

Samaki waliovuliwa jana katika Kizimba cha Ziwani Kurukiri, Kijijini Kigera, Kata ya Nyakatende waliuzwa kwa kiasi cha shilingi 8,500 kwa kilo.

Jimbo la Musoma Vijijini lenye jumla ya Kata 21, lina Kata 18 zilizoko pembezoni mwa Ziwa Victoria. Kwa hiyo, uvuvi ni kazi inayoajiri watu wengi wa Jimboni mwetu.

Wataalamu wa uvuvi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, wakiwemo wa TAFIRI, walishirikiana na NEMC kubaini maeneo mazuri yanayokidhi vigezo vya kufanya uvuvi wa vizimba ndani ya Jimbo letu.

Mbali ya mikopo nafuu iliyotelewa na Serikali yetu kwenye uvuvi wa vizimba, Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini, Prof Sospeter Muhongo anaendelea kuwashawishi wavuvi wa jimboni kwake  kwenda Benki za CRDB na NMB kuchukua mikopo yenye masharti nafuu kwa ajili ya uvuvi wa vizimba. Mbunge huyo ameishawasiliana na Benki hizo mbili kuhusu mikopo hiyo.

Wavuvi na wananchi wa Jimbo la Musoma Vijijini wanaendelea kutoa shukrani nyingi kwa Mhe Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuonyesha njia, kwa vitendo, ya uwekezaji mkubwa kwenye uvuvi wa vizimba nchini mwetu.

Chapisha Maoni

0 Maoni