Mchengerwa azindua mafunzo ya utoaji mikopo kupitia Hatifungani ya Samia

 

Waziri wa Nchi, Ofisi Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. Mohamed Mchengerwa amezindua rasmi mafunzo ya utoaji wa Mikopo kwa Wakandarasi wanaotekeleza Miradi iliyo chini ya TARURA inayotekelezwa na Benki ya CRDB kutokana na fedha zilizokusanywa kwenye mauzo ya Hatifungani ya Miundombinu ya barabara za wilaya (Samia Infrastructure Bond).

Uzinduzi huo umefanyika  tarehe 10 Aprili, 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, jijini Dodoma.

Mhe. Mchengerwa amesema kuwa hiyo ni hatua ya kihistoria ya kuzindua rasmi bidhaa ya kifedha itakayotolewa na Benki ya CRDB kupitia fedha za Hatifungani ya Maendeleo ya Miundombinu ambayo ni mahususi kuwawezesha Wakandarasi wazawa kufanikisha utekelezaji wa Miradi ya TARURA nchini.

"Leo tunasimamia katika ukingo wa kihistoria, leo sio uzinduzi tu wa bidhaa ya kifedha, leo ni uzinduzi wa mapinduzi ya kweli, mapinduzi ya kiuchumi, mapinduzi ya kiutawala na ya kifikra kwa Sekta ya Miundombinu nchini Tanzania."

"Kwa miaka mingi tumeshuhudia Makandarasi wa ndani wakijitahidi, wakijituma kwa bidii lakini wakikwama si kwa sababu hawana uwezo bali ni kwa sababu mazingira hayakuwapendelea," amesema.

Mhe. Mchengerwa ameendelea kubainisha kuwa Hatifungani ya Maendeleo ya Miundombinu  ina maana kubwa katika dhamira ya Serikali ya kuhakikisha utekelezaji wa Miradi ya barabara nchini chini ya TARURA, Makandarasi sasa watapata suluhisho la kifedha litakalowawezesha utekelezaji wa miradi kwa wakati, ufanisi na kwa viwango na ubora vinavyotakiwa.

Aidha, Mhe. Mchengerwa alizindua mfumo wa kidijitali utakaotumika na Makandarasi kuombea mikopo ujulikanao kama 'Samia Infrastructure Portal'  na kusema kuwa mfumo huo utarahisisha upatikanaji wa fedha kirahisi kwa Makandarasi pamoja na kupunguza muda na gharama ya ufuatiliaji kwani unawawezesha kuomba huduma popote walipo.

Kwa upande wake Kaimu Mtendaji Mkuu wa TARURA Mhandisi Edward Amboka amemuahidi Mhe. Waziri kuwa TARURA kwa kushirikiana na Benki ya CRDB wataendelea kuhakikisha Hatifungani hiyo inatumiwa vyema na Makandarasi wazawa katika kutekelezwa miradi Kwa wakati na kwa kuzingatia taratibu na kanuni zilizowekwa.



Chapisha Maoni

0 Maoni