LATRA yaunganisha magari 11,826 mfumo wa VTS

 

Katika kuchukua hatua za kudhibiti mwendo wa kasi kwa magari ya usafirishaji nchini Mamlaka ya Udhibiti Usafiri wa Ardhini (LATRA), imeyaunganisha magari 11,826 kwenye mfumo wa ufuatiliaji mwenendo wa safari (VTS) hadi kufikia Machi 2025.

Hayo yameelezwa leo Jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri wa Ardhini, CPA Habibu J. Suluo katika mkutano wa Wahariri wa Vyombo vya Habari na LATRA, chini ya uratibu wa Ofisi ya Msajili wa Hazina.

 “Kati ya hayo, magari 8,969 yanayotuma taarifa kwenye mfumo mpaka sasa. Pia, wastani wa magari 5,800 yanafanya safari kila siku katika nchi yetu na idadi hiyo huongezeka katika kipindi cha mwisho wa mwaka na hufikia mpaka magari 6,200 yanayofanya safari kwa siku,” amesema CPA Suluo.

Ameeleza kuwa katika magari yasiyotuma taarifa, baadhi hayapo barabarani kutokana na sababu mbalimbali kama, matengenezo ya muda mrefu, ajali, kuungua moto na baadhi yamebadili njia (route) na kuhamia kwenye njia ambazo hazina uhitaji wa kufunga vidhibiti mwendo (VTS).

Mfumo wa VTS unalenga kusimamia matakwa ya usalama wa huduma kama ilivyoelekezwa kwenye Kifungu cha 5(1)(d) na Kifungu cha 6(g) cha Sheria ya Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini, Sura ya 413, LATRA.



Chapisha Maoni

0 Maoni