TARURA kuja na kampeni ya kitaifa ya matumizi sahihi ya barabara

 

Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imesisitiza jamii kutumia barabara kwa kuzingatia matumizi sahihi, na kuwataka baadhi ya wananchi kuacha tabia ya kutupa taka barabarani kwani barabara sio jalala.

Akiongea katika semina ya Waandishi wa Habari wa Mitandao ya Jamii jana Jijini Dar es Salaam Mkuu wa Kitengo cha Mazingira na Jamii wa TARURA, Mhandisi Heladius Makene, amesema kumekuwa na matumizi mabaya ya barabara ambayo hayazingatii uzalendo.

“Wananchi hawapaswi kutupa chupa ama taka za aina yotote barabarani, jambo hilo husababisha uharibifu wa barabara pale taka zinapoziba kwenye mtaro na kuisababishia hasara serikali na jamii inayotumia barabara husika,” alisema Mhandisi Makene na kuongeza,

“Barabara inapoharibika jamii ya eneo hilo wanakosa mawasiliano, wanashindwa kufikia huduma za msingi za kijamii kama vile nyumba za ibada, huduma za afya na elimu pamoja na masoko, pia hata bidhaa bei zake hupanda na kuongeza makali ya maisha.”

Amesema mbali na utupaji taka pia kumekuwapo na mtindo wa kuvamia njia za watembea kwa miguu na hata kwenye service road na kutumika kama sehemu za kufanyia biashara  jambo ambalo ni kosa na si matumizi sahihi ya barabara.

“Wafanyabiashara wanavamia njia za watembea kwa miguu na kufanya biashara na kusababisha kero kwa watembea kwa miguu…wanasahau kwamba sisi sote ni watembea kwa miguu na kuna wakati tuhahitaji kutumia njia hizo,” alisema Mhandisi Makene.

Amesema kwamba, “Kwa mfano Kariakoo wafanyabiashara wamevamia barabara na kusababisha tabu kwa wanunuzi kuingia na magari yao kwenda kununua bidhaa, jambo hili linaathari mapato pengine kungekuwa panapitika wanunuzi wangekuja wengi kuliko ilivyo sasa.”

Amesema kwamba kama hiyo haitoshi kuna watu wanahujumu miundombinu ya barabara kwa kuiba vyuma vya alama za barabarani, kingo za madaraja, taa na hata wengine wamefikia hatua ya kuziponda nguzo za mipaka ili watoe nondo wakauze.

Kwa kutambua tatizo hilo Mhandisi Makene amesema kwamba TARURA kwa kushirikiana na wadau wengine hivi karibuni wanatarajia kuzindua kampeni kubwa ya kitaifa itakayokuwa inajulikana kwa jina la “Barabara Sio Jalala”.

Semina hiyo iliyowahusisha Jumuiya ya Wanahabari Mitandao ya Kijamii Tanzania (JUMIKITA), ilifunguliwa na Meneja wa TARURA Kingamboni Mhandisi Ismail Mafita kwa niaba ya Mtendaji Mkuu wa TARURA Victor Seff.

Chapisha Maoni

0 Maoni