Wathaminishaji wa madini wametakiwa kuwa waadilifu na kutumia
taaluma yao vizuri ili kuepuka makosa madogo madogo.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Usimamizi wa Rasilimaliwatu
na Utawala wa Tume ya Madini, Nsajigwa Kabigi wakati akifungua kikao cha
wathaminishaji wa madini kwa niaba ya Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo kinachoendelea
jijini Dodoma.
Amesema kazi ya uthaminishaji madini inahitaji umakini
mkubwa kwa mthaminishaji kutambua vizuri aina ya madini na kutoa thamani halisi.
"Sasa ikitokea kwa bahati mbaya ukatoa thamani kiasi fulani baadaye ikaenda
kuthaminishwa sehemu nyingine na kuonekana ni tofauti inaharibu sifa yako na uadilifu wako unakuwa na
maswali, hivyo tujitahidi kutumia taaluma zetu vizuri ili hata ikitokea
iwe ni makosa ya kibinadamu na sio uzembe," amesema Kabigi.
Katika hatua nyingine, Kabigi amewataka wathaminishaji
madini kujiendeleza kimasomo ikiwa ni pamoja na kutafuta taarifa mbalimbali
zinazotokana na kazi zao ndani na nje ya nchi pamoja na kushirikishana uzoefu.
"Ni wajibu wetu sisi kama mwajiri kuwaendeleza nyie ili
kuendana na teknolojia mpya na mabadiliko mbalimbali ambayo yamekuwepo,"
amesema Bw. Kabigi.
Awali akizungumza Mkurugenzi wa Ukaguzi na Biashara ya madini CPA. Venance Kasiki amesema lengo la kikao hicho ni kujengeana uwezo na kukumbushana majukumu kwa wathaminishaji madini ili kuendana na teknolojia inavyokuwa.
0 Maoni