Rais Samia ahimiza wanawake viongozi kufanya kazi kwa bidii

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametoa wito kwa wanawake waliobahatika kupata fursa ya elimu na kuwa viongozi kwenye maeneo mbalimbali nchini kuhakikisha kuwa wanafanyakazi kwa bidii, weledi na uadilifu ili kuongeza imani kwa jamii kuhusu umuhimu wa elimu kwa mtoto wakike.

Dkt. Samia ametoa wito huo leo kwenye maadhimishio ya miaka 10 tangu kuanza kwa Mafunzo ya Uongozi kwa Wanawake Tanzania (Female Future Program) yaliyoambatana na Mahafali ya Wahitimu wa Awamu ya 10 ya mafunzo hayo na Mkutano wa 7 wa Uongozi, yaliyofanyika kwenye ukumbi wa The Super Dome Masaki, Dar es Salaam.

Aidha, Rais Samia amewataka wahitimu hao kuwa chachu ya maendeleo katika jamii na kutumia elimu na stadi za uongozi walizopata kunufaisha jamii.

Vilevile, Rais Dkt. Samia ametoa rai kwa wanawake kudhihirisha ushupavu wa uongozi kwenye mashirika na taasisi mbalimbali wanayofanyiakazi na kuwataka kuwa wabunifu na kwenye kazi zao na kuwa waaminifu katika kulipa kodi ili kuwezesha na utekelezaji wa miradi mbalimbali inayogusa maisha ya wananchi.

Kwa upande wa ustawi wa jamii, Rais Dkt. Samia amewausia wanawake kuwa pamoja na elimu na nafasi za uongozi walizonazo, wasiache wajibu wao wa kijamii wa malezi na makuzi ya watoto ili kuwaepusha kujiingiza kwenye mienendo isiyofaa.

Kuhusu uchaguzi mkuu ujao, Rais Dkt. Samia amewahamasisha wanawake wenye sifa na uwezo kujiandikisha kupiga kura na kujitokeza kuwania nafasi mbalimbali za uongozi zitakazowaniwa katika uchaguzi huo.



Chapisha Maoni

0 Maoni