Mallya auawa na kutupwa nje ya nyumba yake

 

Watu wasiojulikana wamemuua Isack Mallya (72) mkazi wa Kijiji cha Umbwe Onana, Kata ya Kibosho Magharibi mkoani Kilimanjaro ambaye ni ndugu wa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kilimanjaro, Patrick Boisafi, na kisha kuutelekeza mwili wake nje ya nyumba yake.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Simon Maigwa amesema tukio hilo limetokea asubuhi ya Desemba 2, 2024 na kueleza kwamba polisi wanafuatilia kujua waliohusika na mauaji hayo.

"Ni kweli kumetokea tukio hilo la mauaji, ambapo huyu mzee amepigwa na kitu kizito kichwani, tunafuatilia tukio hili ili kuwabaini waliohusika na mauaji haya," amesema Kamanda Maigwa.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kilimanjaro, Patrick Boisafi, ambaye ni ndugu wa marehemu ameeleza kusikitishwa na ukatili aliofanyiwa kaka yake na kusema wameliachia Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi ili kubaini waliohusika na sheria ichukue mkondo wake.

"Isack ni kaka yangu, ni mtoto wa baba yangu mkubwa, tumeishi wote mji mmoja na mahali alipouawa ndipo nimekulia hapo, ni jambo la kikatili sana limefanyika katika jamii, lakini naamini jeshi la polisi litafanya bidii kuchunguza matatizo yaliyotokea na kuwatafuta waliohusika na jambo hili ili hatua za kisheria zichukue mkondo wake," amesema Boisafi.

Chapisha Maoni

0 Maoni