Watoto mbaroni kwa kuvunja vioo vya treni ya SGR

 

Jeshi la Polisi nchini limewakamata na kuwahoji watoto wawili kwa tuhuma za uharibifu za kuvunja vioo viwili vya treni ya mwendo kasi inayotumia reli ya kisasa (SGR) kwa kutumia mawe.

Taarifa iliyotolewa na Msemaji wa Jeshi la Polisi DCP David Misime imeeleza kuwa tukio hilo lilitokea Novemba 22, 2024 majira ya mchana katika Kijiji cha Manase Wilaya ya Chamwino katika Jiji la Dodoma wakati Treni ya Mwendo Kasi inapita ikitokea Jijini Dar es Salaam kuelekea Jijini Dodoma.

Baada ya tukio hilo kutokea, Jeshi la Polisi lilifanya msako na kufanikiwa kuwakamata Erasto Michael Richard (16) na Hassan Ezekiel Ndahani (12) wote wakazi wa Kijiji cha Manase Wilaya ya Chamwino.

DCP David Misime amesema chanzo cha kufanya uharibifu huo ni baada ya kuona treni ikipita wakarusha mawe kwa pamoja ili kuona kama mawe waliyorusha yataweza kushindana na mwendo wa treni.

Jeshi la Polisi limetoa wito hasa kwa wananchi wanaoishi maeneo ambayo treni ya kisasa inapita kuendelea kupeana elimu juu ya umuhimu wa kulinda miundombinu ya treni hiyo kwani ipo kwa ajili ya manufaa ya wote.

Chapisha Maoni

0 Maoni