Wananchi wa
Kata za Chala na Ntuchi katika Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi mkoani Rukwa
wameipongeza Serikali kupitia Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA)
kwa ujenzi wa Daraja la mawe la mto Zimba linalounganisha Kata za Chala na
Ntuchi.
Wakizungumza
kwa nyakati tofauti wananchi hao wameishukuru Serikali kwa kujenga daraja hilo
ambalo limewasaidia kusukuma maendeleo yao na kumaliza usumbufu kwa kupita
kwenye maji kila wanapotaka kusafiri kwenda maeneo mengine kwa ajili ya kufuata
huduma mbalimbali za kijamii.
Bw. Oteli
Mwambilija mkazi wa Chala, ameishukuru Serikali kwa ujenzi wa daraja hilo kwani
limekuwa kiunganishi kikubwa kwa wakazi wa kata za Chala na Ntuchi na
limerahisisha shughuli za maendeleo pamoja na shughuli za usafiri na
usafirishaji.
“Tunaishukuru
TARURA kwa ujenzi wa daraja hili, awali kipindi cha mvua mto huu ulikuwa unajaa
sana maji na kusababisha kero kubwa kwa wananchi kuvuka kwenda ng’ambo ya pili,
watu walikuwa wanavuka kwa shida, ng’ombe wetu walisombwa na maji na tulikuwa
tunawakuta mto jirani wa Mfizi, kwakweli tunaishukuru Serikali kwa kujenga
daraja hili kwa sasa tunavuka bila shida yoyote,” alisema.
Naye, Bw.
Samuel Mayesha mkazi wa Chala alisema, baadhi ya vijana walitumia changamoto ya
kukosekana kwa daraja katika mto huo kama fursa kwani walikuwa wanavusha watu
kwa fedha, hapo awali watu walipoteza maisha kwa kukosa daraja lakini sasa hivi
wananchi wanafurahia na daraja limesaidia kusafiri na kusafirisha mazao yao.
Kwa upande
wake, Meneja wa TARURA Wilaya ya Nkasi Mhandisi Karilo Samson, alisema kuwa
ujenzi wa daraja la mawe la mto Zimba lenye urefu wa mita 31 pamoja na barabara
unganishi ya Chala-Ifundwa Km 11.8 limegharimu shilingi milioni 350.
“Barabara
hii tumeifungua haikuwepo hapo awali na tumejenga madaraja (2) ambapo mojawapo
ni hili daraja la mto Zimba kwa kutumia teknolojia ya mawe, baada ya kufungua
barabara tunaendelea na matengenezo ili iweze kupitika majira yote, kwa sasa
mkandarasi yupo “site” anaweka vifusi maeneo korofi yaliyokuwa na utelezi,” alisema.
Alisema,
daraja hilo limekamilika na linatumika kwa ajili ya usafiri na usafirishaji wa
bidhaa hasa mazao kutoka mashambani kwenda sokoni na amewataka wananchi
kuhakikisha wanalitunza ili liweze kudumu na kutumika kwa muda mrefu.
0 Maoni