Muhimbili Mloganzila yawahakikishia wananchi huduma bora

 

Mkurugenzi Mtendaji Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) Prof. Mohamed Janabi amesema uongozi utaendelea kuboresha utoaji wa huduma katika Hospitali ya Muhimbili Mloganzila ili wananchi wapate huduma bora na zinazokidhi matarajio yao.

Prof. Janabi amebainisha hayo alipokuwa akizungumza na Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi katika kikao chake cha 29 kinachofanyika Dar es Salaam ambapo mada mbalimbali zimejadiliwa katika kikao hicho.

Amefafanua kuwa kutokana na usimamizi mzuri na kuendelea kuboresha huduma kwa wateja kwasasa malalamiko yaliyokua yakitolewa na wananchi yamepungua kwa kiasi kikubwa na wananchi wana imani na hospitali hiyo.

“Katika hospitali hii tumeweza kuondoa mtazamo mbaya juu ya Mloganzila kwamba mgonjwa akifikishwa huku anakufa, sasa hivi wananchi wamerejesha imani na hii inajidhihirisha wazi kwani idadi ya wagonjwa wameongezeka mfano katika wagonjwa wa nje awali tulikua tunaona wagonjwa takribani 400 hadi 450 sasa tumefikia wagonjwa 800 hadi 1000 kwa siku,” amefafanua Prof. Janabi.

Prof. Janabi ameeleza kuwa Muhimbili Mloganzila imeendelea kuboresha na kuanzisha huduma mpya za ubingwa bobezi ikiwemo upandikizaji wa nyonga na magoti, upandikizaji figo, upandikizaji uloto, kupunguza uzito, upandikizaji wa meno kwa njia ya kisasa. Huduma hizi pamoja na nyinginezo zimekuwa kivutio kikubwa kwa watu wengi wa ndani na nje ya nchi na hivyo kupunguza rufaa za kwenda nje ya nchi kwa ajili ya matibabu.

Hospitali ya Mloganzila Ilikabidhiwa rasmi kwa Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa usimamizi mwaka 2018 ambapo tangu kipindi hicho maboresho makubwa yamefanyika ikiwa ni pamoja na kusomesha wataalam, kuongeza idadi ya huduma pamoja kuboresha eneo la huduma kwa wateja.

Chapisha Maoni

0 Maoni