Wagonjwa 140 hadi 17 wanaoonwa Mloganzila wana kiharusi

 

Jamii imeshauriwa kuwafikisha hospitalini mapema wagonjwa wenye changamoto za kiharusi ili waweze kupatiwa tiba sahihi kwa wakati kwa lengo la kuepuka madhara zaidi yanayoweza kujitokeza endapo mgonjwa huyo atachelewa kufikishwa hospitalini.

Ushauri huo umetolewa na Naibu Mkurugenzi Mtendaji Hospitali ya Taifa Muhimbili Mloganzila Dkt. Julieth Magandi alipokuwa akitoa elimu kwa wananchi waliojitokeza katika maadhimisho ya siku ya kiharusi duniani yaliyofanyika MNH-Mloganzila.

Dkt. Magandi ameeleza kuwa tatizo la kiharusi ni kubwa na kuongeza kuwa kwa MNH-Mloganzila katika kliniki ya ubongo na mishipa ya fahamu kwa siku wanaona wagonjwa kati ya 140 hadi 170 ambapo kati ya wagonjwa hao asilimia 60 wanabainika kuwa na kiharusi.

 “Baada ya kuona ukubwa wa tatizo la kiharusi Muhimbili Mloganzila tumeamua kuboresha huduma za magonjwa ya kiharusi kwa kuanzisha kitengo maalum cha kuhudumia wagonjwa wenye kiharusi ambapo tumeweka vifaa tiba vya kisasa vyenye uwezo wa kufuatilia mwenendo wa mgonjwa kwa wale wagonjwa ambao wamelazwa wodini.”

Kwa Upande wake Daktari Bingwa Mbobezi wa Magonjwa ya Ubongo na Mishipa ya Fahamu MNH-Mloganzila Dkt. Mohamed Mnacho amesema kuwa ugonjwa wa kiharusi ni moja kati ya magonjwa yanayoongoza kwa kusababisha vifo na ulemavu duniani.

Pamoja na hayo, amesema takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) zinaeleza kuwa zaidi ya watu milioni 12 duniani wanatatizo la kiharusi ambapo kati ya hao watu milioni 6 hupoteza maisha kutokana na ugonjwa huo kwa mwaka.

Pamoja na hayo ameitaka jamii kuacha baadhi ya tabia ambazo zinaweza kuchangia watu kupata ugonjwa wa kiharusi ikiwemo uvutaji wa sigara, unywaji wa pombe kupita kiasi, uzito mkubwa pamoja kutokufanya mazoezi.

Siku ya kiharusi Duniani huadhimishwa Oktoba 29 kila mwaka ambapo kwa Muhimbili Mloganzila imeadhimisha siku hiyo kwa kutoa huduma mbalimbali bure ikiwemo upimaji wa shinikizo la damu, elimu ya lishe pamoja na ugonjwa wa kiharusi.

Chapisha Maoni

0 Maoni