SMZ kujenga uwanja mpya wenye viwango vya FIFA

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inajipanga kujenga uwanja mkubwa wa michezo utakaokuwa na vigezo vinavyokubalika na Shirikisho la Soka Duniani FIFA pamoja na Shirikisho la Soka Barani Afrika CAF.

Rais Dk. Mwinyi ameyasema hayo leo tarehe 25 Septemba 2024 Ikulu, Zanzibar alipokutana na viongozi na wachezaji wa Klabu ya Simba ya Dar es Salaam waliofika kumsalimia kabla ya mchezo wao wa kesho dhidi ya Azam utakaochezwa Uwanja wa Amani Complex, majira ya saa mbili usiku.

Aidha, Rais Dk.Mwinyi amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha michuano ya soka inayowashirikisha wachezaji wanaocheza ligi za ndani (Chan) na ile ya michuano ya soka ya mataifa ya Afrika kwa timu za taifa (AFCON), kuwa Zanzibar ni sehemu itakayochezwa michezo hiyo.

Halikadhalika, Rais Dk. Mwinyi ameelezea dhamira ya Simba ya kujenga kituo cha kuwaendeleza vijana katika mchezo wa soka hapa Zanzibar (soccer academy) kuwa ni jambo jema na kuwaahidi Serikali ipo tayari kuwaunga mkono kwa kuwapa eneo la ujenzi wa kituo hicho.

Naye, Mwenyekiti wa Klabu ya Simba, Murtaza Mangungu amemuhakikishia Rais Dk. Mwinyi kwamba Klabu hiyo ipo tayari kuitangaza Zanzibar kimataifa kupitia utalii wa michezo.

Vilevile, amepongeza juhudi za Rais Mwinyi kuendeleza viwanja vya michezo kila wilaya Unguja na Pemba, kwani michezo ni nyezo muhimu ya kukuza umoja, furaha na upendo miongoni mwa wananchi.


Chapisha Maoni

0 Maoni