Rais wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi amesema
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inajipanga kujenga uwanja mkubwa wa michezo
utakaokuwa na vigezo vinavyokubalika na Shirikisho la Soka Duniani FIFA pamoja
na Shirikisho la Soka Barani Afrika CAF.
Rais Dk. Mwinyi
ameyasema hayo leo tarehe 25 Septemba 2024 Ikulu, Zanzibar alipokutana na
viongozi na wachezaji wa Klabu ya Simba ya Dar es Salaam waliofika kumsalimia
kabla ya mchezo wao wa kesho dhidi ya Azam utakaochezwa Uwanja wa Amani
Complex, majira ya saa mbili usiku.
Aidha, Rais
Dk.Mwinyi amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha michuano ya soka
inayowashirikisha wachezaji wanaocheza ligi za ndani (Chan) na ile ya michuano
ya soka ya mataifa ya Afrika kwa timu za taifa (AFCON), kuwa Zanzibar ni sehemu
itakayochezwa michezo hiyo.
Halikadhalika,
Rais Dk. Mwinyi ameelezea dhamira ya Simba ya kujenga kituo cha kuwaendeleza
vijana katika mchezo wa soka hapa Zanzibar (soccer academy) kuwa ni jambo jema
na kuwaahidi Serikali ipo tayari kuwaunga mkono kwa kuwapa eneo la ujenzi wa
kituo hicho.
Naye,
Mwenyekiti wa Klabu ya Simba, Murtaza Mangungu amemuhakikishia Rais Dk. Mwinyi
kwamba Klabu hiyo ipo tayari kuitangaza Zanzibar kimataifa kupitia utalii wa
michezo.
Vilevile,
amepongeza juhudi za Rais Mwinyi kuendeleza viwanja vya michezo kila wilaya
Unguja na Pemba, kwani michezo ni nyezo muhimu ya kukuza umoja, furaha na
upendo miongoni mwa wananchi.
0 Maoni