Kamishna
Msaidizi wa Uhifadhi Hifadhi ya Taifa Milima Udzungwa, Theodora Aloyce, amesema
wananchi wanaoishi kando ya Hifadhi ya Milima Udzungwa wamekuwa wanufaikaji
wakubwa kiuchumi kutokana na kufanya biashara ya utalii kwa kuuza mazao ya
utalii ambayo yamekuwa kivutio kikubwa kwa wageni wanaotoka nje, ikiwemo utalii
wa vyakula vya asili na matunda kama madafu, ambayo yameongeza thamani ya
Hifadhi hiyo.
Kamishna
Msaidizi Aloyce ameyasema hayo jana wakati akiwapokea wageni kutoka Halmashauri
ya Mji wa Masasi, wakiwemo Madiwani pamoja na wakuu wa idara, waliotembelea
Hifadhi ya Milima Udzungwa, lengo likiwa ni kujionea upekee wa Hifadhi hiyo yenye maporomoko ya maji ya mita 170,
spishi za mimea, wanyamapori wa kipekee, na ndege wa ajabu.
“Katika
vijiji vyetu tumeweka mahusiano mazuri baina yetu sisi wahifadhi pamoja na
wananchi wakazi wa hapa. Wamejifunza namna ya kuongeza thamani ya utalii wa
vyakula vya asili, wamekuwa wanauza vikapu, bangili pamoja na madafu ambapo
wageni wengi, hususan watalii kutoka nje, wanafurahia madafu ya Udzungwa
kutokana na historia ya matunda hayo,” alisema Afande Aloyce.
Kwa upande
wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Masasi, Mhe. Hashimu Namtumba,
alisema lengo la wao kutembelea Hifadhi hiyo ni kuunga mkono jitihada za Mhe.
Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuutangaza utalii wa maliasili za Taifa
pamoja na kuwa mabalozi wazuri katika kuhifadhi na kutunza rasilimali za nchi.
“Kwakweli ni
Hifadhi nzuri sana. Tumefurahia kujionea maporomoko ya maji. Mengi tumekuwa
tukisikia tu, lakini leo tumepata historia na kujua baadhi ya wanyama, ikiwemo
nyani wa Ngolanga wanaopatikana hapa tu katika ulimwengu wote, pamoja na ndege
wengi wa kipekee,” alisema Mhe. Namtumba.
Naye Kaimu
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Masasi, Bi. Remada Mbowe, alielezea namna upekee
wa Hifadhi ya safu ya Milima Udzungwa
utakavyoenda kuimarisha mawazo yao katika utendaji wa shughuli zao za kila
siku, kwani mazingira yake yanaburudisha na yanapunguza msongo wa mawazo kwa
mtu yeyote atakayefika katika mandhari ya Hifadhi hiyo.
“Kwakweli
katika Hifadhi hii tumeona vitu vizuri.
Mimi binafsi nilipofika katika haya maporomoko ya maji nilishindwa kujizuia,
nilikimbilia haya maji, kwakweli ni mazuri sana. Watanzania sasa waone haja ya
kutembelea Hifadhi hii kwani nimejionea mengi na mengine yanajenga akili zetu
upya,” alisema Bi. Remada.
Hifadhi ya
Taifa ya Milima Udzungwa inatambulika kama Hifadhi pekee yenye uzuri unaovutia
bionuai kubwa. Maporomoko yake ya maji yenye mita 170 yanaifanya Hifadhi hiyo
kuwa na umuhimu mkubwa katika uhifadhi wa maji ambayo ni chanzo muhimu cha mito
inayohudumia katika maeneo ya karibu.
Na: Zainab
Ally-Udzungwa
0 Maoni