Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk.
Hussein Ali Mwinyi, amelishauri Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) kuongeza
safari za kimataifa kupitia Zanzibar kwa lengo la kukuza utalii pamoja na
kufungua kisiwa cha Pemba kiutalii kutokana na vivutio lukuki ambavyo
vinahitaji kutangazwa.
Rais Dk. Mwinyi ameyasema hayo alipomwakilisha Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakati wa
Uzinduzi na Mapokezi ya ndege mpya ya Boeing 787-8 Dreamliner, iliyowasili
nchini leo tarehe 20 Agosti 2024 katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid
Amani Karume.
Ndege hiyo mpya, ambayo ni ya 16 kununuliwa na Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imetoka moja kwa moja Marekani, imeigharimu
shilingi bilioni 300.
Halikadhalika, Dk. Mwinyi amesema Serikali itaendelea
kuwekeza katika sekta ya anga kwani ni njia muhimu ya kufungua milango ya
kiuchumi na kuunganisha nchi na mataifa mengine kimaendeleo.
Aidha, amebainisha kuwa kuimarisha Shirika la Ndege la
Tanzania (ATCL) ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2020-2025.
Kwa upande mwingine, Dk. Mwinyi amezipongeza juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan za kuendeleza na kuimarisha Shirika la Ndege la Tanzania, kwani limeijengea heshima kubwa nchi na kuwa miongoni mwa mashirika yenye ndege nyingi kwa nchi za Kusini mwa Afrika.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi akiwa na Mkewe Mama Mariam Mwinyi kwenye ndege mpya ya Boeing 787-8 Dreamliner, iliyowasili nchini leo tarehe 20 Agosti 2024 katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume.
0 Maoni