Wageni zaidi ya 800 kutoka Chama cha Wafanyakazi wa Serikali
na Afya (TUGHE) wamefanya ziara ya kihistoria katika eneo la hifadhi ya
Ngorongoro leo tarehe 29 agosti, 2024.
Ziara hiyo ambayo imefanyika baada ya wajumbe wa TUGHE
kumaliza semina iliyofanyika jijini Arusha kuanzia tarehe 26/08/2024 ina lengo la kuwaleta pamoja waajiri na
wafanyakazi ili kupata uwelewa wa pamoja, kujadili na kutatua changamoto
mbalimbali zinazojitokeza mahala pa kazi.
Akiongoza ujumbe huo Mwenyekiti wa TUGHE Taifa Bw. Joel George
Kaminyoge amesema lengo la ziara yao ni kutoa hamasa ya utalii wa ndani na
kuunga mkono jitihada za Mhe. Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.
Samia Suluhu Hassan katika kukuza utalii ambapo ziara hiyo imewapa fursa
wanachama wao kujionea vivutio vya
kipekee vinavyopatikana hifadhi ya Ngorongoro.
“Leo tumekuja na wanachama zaidi ya 800 kutembelea Kreta ya
Ngorongoro kujionea moja kati ya vivutio bora vya dunia ambavyo ni sehemu ya
urithi wa dunia, Tunaamini kwamba ziara
yetu italeta tija na hamasa kwa wakuu wa taasisi kuwa na utaratibu wa
kuwapeleka watumishi wao kufanya utalii wa ndani katika vivutio mbalimbali
nchini,” alisema Bw. Kaminyoge
Akiwapokea wageni hao, Meneja wa huduma za Utalii na masoko
wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Bi.Mariam Kobelo, alisema kwamba Mamlaka
hiyo ipo tayari kuendelea kupokea makundi mbalimbali ya wageni na
kuwahakikishia kuwa wanapata huduma bora ili kuendelea kutqngaza hifadhi
hiyo na kuimarisha utalii ndani.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Tanzanite Cooperates L.t.d
aliyeratibu ziara hiyo Bi. Elina Mwangomo, ameleza kuwa kwa sasa kuna ongezeko
kubwa la watalii wa ndani hali inayoongeza hamasa kwa wadau wa utalii kuendelea
kuboresha huduma zao huku akieleza kuwa Ngorongoro imekuwa moja kati ya eneo ambalo
linapendwa zaidi na wageni na watalii kutoka maeneo mbalimbali ya nchi.
“Natumia fursa hii kumshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu
Hassan kwa kutuwekea mazingira wezeshi kwani baada ya filamu ya Royal Tour
kumekuwa na mwamko mkubwa wa utalii ambao umetusaidia sisi wadau wa Utalii
kupata fursa ya kupokea watalii wengi zaidi, mfano leo tumeweza kuingia
Ngorongoro na watalii wa ndani zaidi ya 800 na naamini makundi haya yataendelea
kuja kwa wingi,” aliesema Bi. Elina
Mwangomo.
Bi. Jackline Ngoda ambaye ni mmoja kati ya wanachama
waliotembelea Hifadhi hiyo ameonesha kufurahishwa na ziara hiyo baada ya
kujionea Wanyama mbalimbali ikiwepo wanyama wakubwa watano (Big 5) wakiwa
katika maeneo yao ya asili.
“Kwa ujumla tumeona Wanyama mbalimbali, wakiwemo Simba,
Nyati, Tembo, Swala, nyumbu, viboko, pundamilia na wengine wengi, tumeweza
kuona uzuri wa kipekee wa Kreta ya Ngorongoro na napenda kuwaambia watanzania
wenzangu waje kutembelea Ngorongoro na kujionea uzuri wake wa asili,” alisema
Jackline.
Ziara hii ni sehemu ya juhudi za TUGHE kuwaleta pamoja waajiri na wafanyakazi wa taasisi za Serikali kupata nafasi ya kujifunza na kujenga uhusiano mzuri na ushirikiano nje ya mazingira rasmi ya kazi.
0 Maoni