Naibu Waziri Mhe. Sangu apata mapokezi makubwa mkoani Rukwa

 

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora na Mbunge wa Jimbo la Kwela, Mhe. Deus Sangu amewahakikishia  wananchi kuwa  atafanya kazi kwa weledi na uaminifu wa hali ya juu  huku  akimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa heshima kubwa  aliyowapa  wananchi wa Jimbo la Kwela na Mkoa wote wa Rukwa  kwa kumteua yeye  kuwa Naibu Waziri wa Ofisi yake.

Aidha, Mhe. Sangu amewashukuru wananchi wote  wa Mkoa wa Rukwa kwa mapokezi makubwa  waliyompa mara baada ya kuwasili Mkoani humo, ikiwa ni ziara yake ya kwanza tangu alipoteuliwa kushika wadhifa huo.

Mhe. Sangu  ametoa kauli hiyo  kwa nyakati tofauti wakati akizungumza na Watumishi pamoja na wananchi  katika  Kata ya Kanda na  Kaengesha  kwenye mikutano ya hadhara iliyofanyika  kwenye Vijiji vitano  vya Jimbo la Kwela , Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga  Mkoani  Rukwa.

Amesema Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan amewaheshimisha wananchi wa Mkoa wa Rukwa kwa kumteua yeye ili aweze kumusaidia kuwahudumia Watanzania katika masuala ya utumishi na utawala bora.

"Naomba niwaahidi katika najukumu yangu haya mapya nitakuwa mnyenyekevu, mchapakazi, mweledi na mwaminifu katika kutekeleza majukumu yangu ya kumsaidia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.George Simbachawene " amesema Mhe. Sangu.

Ameongeza "Nawashukuru pia wananchi wa Kwela kwa kuniamini na kunituma Bungeni ili nikawesemee changamoto zinazowakabili hii imepelekea Rais Samia kuweza kuniona na kuniteua kushika Wadhifa huu.

Katika hatua nyingine Mhe. Sangu ametumia fursa hiyo kumshukuru Mhe.Rais kwa kutekeleza miradi mingi ya maendeleo katika Jimbo la Kwela ikiwemo ujenzi wa zahanati, barabara, maji pamoja na umeme.

Mhe. Mhe. Sangu amewahakikishi wananchi hao kuwa  “Mambo mazuri zaidi yanakuja, Rais Samia amesema anataka kuiona  Kwela   yenye nuru kiuchumi,” amesisitiza Mhe.Sangu.

Amesema Mhe.Rais anawapenda sana wananchi wake hususan wa Mkoa wa Rukwa ndio maana ameongeza bei ya mazao ya mahindi   hadi Sh.700 kwa kilo moja ili kuhakikisha wananchi wa Kwela wananufaika kiuchumi kupitia kilimo chao.

Hata hivyo Mhe.Sangu ameowaonya wananchi wake wasithubutu kuuza mazao yote la sivyo kufikia Mwezi Januari mwakani watakumbwa na baa la njaa.

Kwa upande wake Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Rukwa, Mhandisi, Daudi Sebiga ametumia fursa hiyo kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kumteua Mhe.Deus Sangu kwani Mchapakazi na Mwaminifu wa kiwango cha hali ya juu sana.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.Deus Sangu akizungumza na Elus Homera mara baada ya kuwasili katika mkutano wa Hadhara uliofanyika katika Kata ya Kanda, ikiwa ni ziara ya kwanza tangu alipoteuliwa kushika wadhifa huo.

Sehemu ya wananchi wa Kata ya Kanda, Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga Mkoani Rukwa wakimshangilia kwa shwange Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe.Deus Sangu mara baada ya kuwasili, ikiwa ni ziara yake ya kwanza tangu alipoteuliwa kushika wadhifa huo.

Chapisha Maoni

0 Maoni