Banda la Maliasili na Utalii lazidi kuwa kivutio Maonesho ya Nane Nane

 

Ushiriki wa Wizara ya Maliasili na Utalii imekuwa kivutio kikubwa katika maonesho ya 30 ya Kimataifa ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ya Nane Nane yanayoendelea kufanyika kitaifa Jijini Dodoma katika viwanja vya Nzuguni.

Uwepo wa vivutio vya wanyamapori hai, utambulisho wa banda (branding) pamoja na vivutio vya Screen kubwa ya utangazaji kwenye magari ya TANAPA, na shughuli za kiutamaduni kupitia gari la Makumbusho ya Taifa vimekuwa vikiwavutia wananchi wengi kutembelea banda hilo. Aidha, washiriki kutoka Idara na taasisi chini Wizara wamejipanga kutoa elimu ya uhifadhi na utalii pamoja na kuhamasisha wananchi kutembelea maeneo ya vivutio vya utalii nchini.

Akizungumza kwenye maonesho hayo ndani ya Banda la Wizara, Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Kitengo cha Maendeleo ya Utalii ambaye pia, ni Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi kwa upande wa wizara, Bw. Juvenile Jaka Mwambi, amesema ‘’ukifika kwenye banda hilo mbali na wanyamapori hai, pia utajifunza na kuelezewa fursa mbalimbali za uwekezaji ndani ya Sekta ya maliasili na Utalii pia utapata chakula cha aina mbalimbali ikiwemo nyamachoma ya wanyamapori.’’

Amesema pia kuna makumbusho inayotembea ambayo itafanya wananchi kujifunza mambo mbalimbali ya kale.

"Tunawakaribisha sana wananchi kuja kujifunza mambo mengi ambayo hutaweza kuyapata kirahisi lakini kwenye maonesho haya ya Nanenane utayapata."

Kwa siku ya leo, watu mbalimbali wametembelea banda hilo akiwemo Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini, Bi. Bure Nassibu pamoja na Mkurugenzi wa Mafunzo na Takwimu, Dkt. Edward Kohi.

Vilevile, kwa mujibu wa taarifa za takwimu za wananchi waliotembelea banda la Wizara kwa  siku ya ya leo kwa ujumla, wananchi 3,053 wamembelea banda hilo, ambayo ni idadi kubwa kuliko ya waliotembelea siku ya jana ambayo ni wananchi 813  sawa na ongezeko la asilimia 73 suala ambalo linaonesha namna gani Wizara hiyo imeendelea kuwa kivutio katika maonesho hayo.

Na. John Bera- Dodoma

Chapisha Maoni

0 Maoni