Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-TAMISEMI anayeshughulikia
miundombinu Mhandisi Rogatus Mativila amefurahishwa na viwango vya ujenzi wa
miradi ya barabara za lami zinazosimamiwa na Wakala ya Barabara za Vijijini na
Mijini (TARURA) mkoani Dodoma.
Mhandisi Mativila ameyasema hayo mara baada ya kumaliza
ziara yake ya kikazi ya kukagua uimara wa barabara zinazosimamiwa na TARURA
ambapo alitembelea miradi minane.
Alisema barabara zote hizo zimejengwa kwa fedha za tozo na mfuko
wa maendeleo wa barabara ambazo hutolewa na serikali kwaajili ya kuboresha miundombinu
ya barabara hususani maeneo ya mijini.
“Nimefurahishwa na viwango vya barabara hizi ambazo
zinasimamiwa na TARURA pamoja na makandarasi waliojenga barabara mkoani Dodoma,
wamefanya kazi nzuri na hata kwa kuangalia kwa macho barabara zote zipo kwenye
viwango vizuri hata wakazi wanaoishi jirani na barabara hizi unaona
wanavyofurahia barabara hizi.”
Aliongeza kusema kwamba anaishukuru Serikali ya Awamu ya
Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha kwaajili ya
kuboresha miundombinu ya barabara hususani barabara za mijini.
"Sisi tunashukuru sana kwa kutupa maisha bora kupitia
miundombinu ambayo Mhe. Rais aliamua kuongeza fedha na kuhakikisha zinajengwa
barabara kwa kiwango cha lami," aiongeza Mha. Mativila.
Aidha, akiwa kwenye barababa inayounganisha barabara ya
kutoka Dodoma kwenda Singida (Nala)
inayoelekea kiwanda cha mbolea cha Itracom Fertilizer Limited yenye
urefu wa Km. 5, Naibu Katibu Mkuu huyo alisema kwenye sera ya viwanda zipo
fedha ambazo serikali imeongeza fedha za tozo ambazo zinatumika katika
maendeleo ya miundombinu inayoenda
kwenye viwanda ambapo viwanda hivyo vinatoa
ajira kwa watanzania pia kwa mbolea inayotengenezwa hapo inauzwa kwa bei
nafuu.
"Barabara hii inasaidia kiuchumi na kijamii kwani
maeneo jirani na kiwanda hiki yamepimwa hivyo inawarahisishia usafiri pia
wakazi wa Dodoma wanapata ajira kupitia kiwanda hiki," alisisitiza.
Hata hivyo Mha. Mativila alisema barabara hiyo inayoruhusu
magari yenye kubeba mizigo yenye uzito wa Tani 56 na hivyo kurahisisha
usafirishaji wa malighafi kutoka nje ya kiwanda na pia mbolea toka kiwandani na
kuwafikia wananchi kwaajili ya kilimo.
Naye, Msimamizi wa miradi wa barabara ya Swaswa-Mpamaa yenye
urefu wa Km. 8.7 Mhandisi Atuletile Ngailo amesema mradi huo umeweza kukuza uchumi
wa wakazi hao pia umewapunguzia umbali kwa kutumia barabara hiyo.
Kwa upande wake Meneja wa TARURA wilaya ya Dodoma Mhandisi
Emmanuel Mfinaga alisema barabara zilizojengwa mjini hapa zimekuwa mkombozi kwa
wananchi kwani maeneo mengi hayakuwa na barabara kabisa na hivyo ameishukuru
serikali kwa kuendelea kupeleka fedha za kutengeneza na kuboresha barabara
wilayani Dodoma.
Bi. Rehema Malongo Mkazi wa Nala alisema wanaishukuru serikali kwa kujenga barabara ya lami kuelekea maeneo ya viwandani kwani imewarahisihia usafiri wa mazao yao na pia vijana wao kupata ajira kupitia kiwanda hicho cha mbolea.
Na. Catherine Sungura, Dodoma
0 Maoni