Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa
Umma na Utawala Bora na Mbunge wa Jimbo la Kibakwe, Mhe. George Simbachawene
ameonya matumizi ya gari ya wagonjwa
(ambulance) iliyotolewa na Serikali
katika Kituo cha Afya cha Ipera lisitumike kubeba nyumba ndogo badala ya
itumike kwa ajili ya malengo
yaliyokusudiwa.
Pia amesema gari hiyo isitumike kibiashara kwa kuanza kubeba
abiria au mazao bali itumikwe kwa ajili ya kuwahudumia wagonjwa hususani akina
mama wajawazito.
Waziri Simbachawene ametoa kauli hiyo leo wakati wa hafla ya
kukabidhi gari hiyo mara baada ya kufanya mkutano wa hadhara katika Kata ya
Ipera, Kibakwe iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa jijini Dodoma
ambapo amewataka wananchi wawe walinzi wa gari hiyo.
“Msisitizo wangu gari hii ya wagonjwa ni gari la Serikali na
ni gari ya wananchi hivyo nitawashangaa kuiona gari hii ikibeba abiria au
magunia ya mazao, Naombeni kila mmoja wetu awe mlinzi wa gari hii kwani ni yetu
sote,” amesisitiza Mhe.Simbachawene.
Amefafanua kuwa azma ya Serikali ya kutoa gari hiyo ni
kuhakikisha inasaidia kuwafikisha wagonjwa katika hospitali ya Rufaa kwa muda
muafaka pale ambapo mgonjwa anapewa rufaa ya matibabu.
“Tunataka tukiliona gari hili likiwa linatembea barabarani
liwe limebeba mgonjwa au linaenda kumfuata mgonjwa na sio vinginevyo,”
amesisitiza Mhe. Simbachawene.
Katika hatua nyingine, Mhe. Simbachawene amesema wanaangalia utaratibu wa kuwatafuta
madereva wa gari za wagonjwa viliko vituo vya afya ili magari hayo yasikae makao makuu ya
Halmashauri ya wilaya badala yake magari
hayo yakae kwenye maeneo husika ambako
kuna vituo vya afya.
Amesema hali hiyo itasaidia kutoa huduma ya haraka kwa
wagonjwa mara tu pale gari linapohitajika
Aidha, Mhe. Simbachawene ametoa wito kwa akina mama
wajawazito kuwahi katika vituo vya afya mara waonapo dalili za kuanza kwa
uchungu ili kuepuka vifo visivyo vya lazima huku akiwasihi manesi kuwahudumia
wagonjwa kwa upendo kama viapo vyao vinavyowataka.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa, Mhe. George Fuime amesema atahakikisha wanafuatilia kwa ukaribu matumizi ya gari hilo ili liweze kuwa msaada kwa wananchi wote wa Kata ya Ipera na wilaya nzima ya Mpwapwa.
Na. Mwandishi Wetu - Dodoma
0 Maoni