Kamati ya Kitaifa ya Ushauri kuhusu utekelezaji wa Programu
ya Kizazi chenye Usawa imeridhika na utekelezaji wa Programu hiyo Wilayani
Chamwino hasa katika kuwezesha jamii kwenye malezi, Makuzi na Maendeleo ya
Awali ya Mtoto ili Mama apate muda wa kuendelea shughuli za kiuchumi.
Hayo yamebainika wakati wa siku ya pili ya ziara ya Kamati
hiyo mkoani Dodoma yenye lengo la kufuatilia utekelezaji wa Programu hiyo.
Akizungumza jana kwa niaba ya Mwenyekiti wa Kamati hiyo
Nangi Masawe amesema uwepo wa Vituo vya Malezi na Makuzi inatoa fursa kwa
Wanawake kuendeleza shughuli zao za kiuchumi kwani wakikosa sehemu sahihi za
kuwaacha watoto wao wanaweza kupatwa na madhira ya ukatili na wao pia kukosa
fursa mbalimbali za kupata kipato na kufikia Usawa wa kijinsia katika uchumi.
Ameongeza kuwa lengo kubwa la Programu ya Kizazi chenye
Usawa sio kumwezesha mwanamke kifedha tu kupata mtaji wa biashara bali kuweka
mazingira wezeshi ya kumpunguzia adha katika sekta mbalimbali zikiwemo
upatikanaji wa maji, Nishati ya umeme, Nishati safi ya kupikia na uwezeshaji
katika elimu itakayomsaidia kuelekea katika Kizazi chenye Usawa nchini.
"Jambo mnalofanya hapa Walezi wa kituo hiki ni la heri
sana na hii ni dhana nzuri katika kuwasaidia watoto wetu katika malezi na pia
kutoa fursa kwa Wanawake kuendelea na shughuli za kiuchumi ili tuweze kufika
Kizazi chenye Usawa kama Mhe. Rais alivyoweka ahadi Kimataifa,"
alisisitiza Nangi
Naye Mjumbe wa Kamati hiyo Carolyn Kandusi amesema kuwepo wa
vituo vya Malezi sio inampunguzia mzazi mzigo wa malezi kwa Mtoto na kukosa
muda wa Kufanya shughuli za kiuchumi bali inasaidia watoto kupata Malezi
stahili wakiwa katika vituo husika, hivyo itasaidia kujenga familia, Jamii na
Taifa lenye imara katika malezi kwa watoto.
"Nimefurahishwa sana kuona juhudi za Wilaya hii ya
Chamwino katika kuhakikisha inawasaidia Wanawake kupata sehemu sahihi za kuwaacha
watoto wao wakipata Malezi na wao kufanya shughuli zingine za kiuchumi, Sisi
kama Kamati tutamshauri Mhe. Rais Vituo hivi viweze kuwepo katika Shule zote za
Msingi ili kusaidia Jamii," amesema Carolyn.
Akielezea Programu ya Kizazi chenye Usawa wakati wa ziara
hiyo Mratibu wa Programu hiyo kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia,
Wanawake na Makundi Maalum Leah Ipini amesema kuwa Programu hiyo inalenga
kuleta haki na usawa kwa wanawake na wanaume hivyo itapelekea kupungua kwa
vitendo vya ukatili, fursa sawa katika matumizi ya Teknolojia, uhuru na haki
kwa Wanawake, uwekezaji wenye mlengo ya kijinsia, matumizi ya Nishati safi,
upatikanaji wa maji safi na salama karibu na kutatua changamoto mbalimbali
zilizokuwa zinamfanya mwanamke akose muda mwingi wa kufanya shughuli za
kiuchumi na kujiletea maendeleo.
Naye mmoja ya mzazi wanaufaika kwa Kituo cha Malezi na Makuzi ya Awali ya Mtoto katika Shule ya Msingi Chamwino Agness Joram ameishukuru Serikali kwa kuwezesha upatikanaji wa vituo hivyo katika maeneo yao kwani vinawasaidia kupata muda wa kufanya shughuli zao za kiuchumi na kuwapa watoto wao Malezi ya Awali wanayostahili.
Na. WMJJWM- Dodoma
0 Maoni