Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki (Mb)
amekutana na kufanya mazungumzo na Uongozi wa juu wa Kampuni ya IFEMA ya
Madrid, Hispania inayojihusisha na uandaaji wa Onesho linaloongoza duniani la
Feria Internacional de Turismo (FITUR) lengo ikiwa ni kuangalia namna bora ya
kuboresha ushiriki wa Tanzania katika Onesho hilo na kuitangaza zaidi Tanzania
katika soko la Kimataifa.
Akizungumza katika kikao hicho kilichofanyika jijini
Barcelona, Hispania jana Juni 10,2024 Waziri Kairuki amesema kuwa ushiriki wa
Tanzania kwenye Onesho hilo utaifanya Tanzania kujulikana zaidi Kimataifa.
Aidha, amewahakikishia waandaaji hao kuwa Tanzania ina
dhamira ya kuendelea kushiriki ipasavyo kwenye onesho hilo na iko tayari
kupokea maoni na ushauri wa namna ya kuweza kuboresha zaidi ushiriki wake ili
iweze kufanikiwa kujitangaza katika soko la Kimataifa hasa Hispania na Latin
Amerika.
Mwaka 2023 Hispania ilishika nafasi ya pili kwa kuwa eneo
linalotembelewa zaidi duniani kwa kuingiza watalii wa kimataifa milioni 85,
ikifuatiwa na Marekani (watalii milioni 66), Italia (watalii milioni 57) na
Türkiye, ambayo ilifunga tano bora kwa kuwa na watalii milioni 55 wa kimataifa.
Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya IFEMA, Bi. MarÃa
Valcarce amesema kuwa onesho la FITUR ni soko kubwa la kimataifa la utalii
linalopata washiriki takribani 152,000 ambao ni waendesha watalii, mashirika
mbalimbali na wageni takribani 92,000.
Aidha, amesema IFEMA iko tayari kushirikiana na Tanzania
kuangalia namna bora ya kufanikisha ushiriki wake katika maonesho yajayo.
“Tunataka kuitangaza Afrika kupitia FITUR na kuwaleta watu
wa Hispania kuijua Afrika na mnyororo mzima wa biashara katika sekta ya utalii,”
amesisitiza Valcarce.
Waziri Kairuki yupo jijini Barcelona Hispania kwa ajili ya kushiriki katika mkutano wa 121 wa Baraza Tendaji la Shirika la Utalii Duniani utakaofanyika kesho Juni 11, 2024 jijini Barcelona, Hispania.
Na Mwandishi Wetu- Barcelona, Hispania
0 Maoni