Wizara ya Maliasili na Utalii Kupitia Shirika la Hifadhi za
Taifa (TANAPA) katika kipindi cha Mwaka 2020/2021 na Mwaka 2022/2023 ilitumia
jumla ya Shilingi 144,268,404 kujenga nyumba ya Mganga na Nesi (mbili kwa moja)
pamoja na kutengeneza samani kwa ajili ya Kituo cha Afya Hunyari, Wilayani
Bunda Mkoani Mara.
Haya yamebainishwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii
Mhe. Dunstan Kitandula(Mb) alipokuwa akijibu swali la Mhe. Boniface Mwita
Getere(Mb) aliyetaka kujua TANAPA itamalizia lini jengo la upasuaji katika Kituo cha Afya
Hunyari wilayani Bunda.
Mhe. Kitandula aliongeza kuwa Wizara ya Maliasili na Utalii
kupitia TANAPA imeweka utaratibu wa kufadhili miradi ya ujirani mwema kwa
maeneo yanayozunguka Hifadhi za Taifa.
Vile vile, ili kuendelea kunufaika na miradi ya ujirani mwema ambayo ni sehemu ya manufaa ya shughuli za Uhifadhi na Utalii, “Natoa rai kwa wananchi wa Kijiji cha Hunyari Wilayani Bunda kutumia utaratibu uliowekwa na TANAPA katika kufadhili miradi ya ujirani mwema kwa kutuma maombi rasmi kuhusiana na umaliziaji wa jengo hilo la upasuaji,” alisema Mhe. Kitandula.
Na. Anangisye Mwateba-Bungeni Dodoma
0 Maoni