Kikundi cha Maafisa na Askari wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania, Vyombo vya Usalama na Taasisi mbalimbali za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kilichoshiriki Zoezi la 13 la Medani la Nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki "FTX Ushirikiano Imara 2024" lililofanyika nchini Rwanda, kimekabidhi bendera ya taifa mara baada ya kurejea nchini leo tarehe 23 Juni 2024.
Akizungumzia kwa niaba ya Mkuu wa Majeshi Jenerali Jacob
John Mkunda, Mkuu wa Kamandi ya Vikosi chini ya Makao Makuu ya Jeshi Meja Jenerali
Iddi Said Nkambi amewataka Maafisa na Askari walioshiriki zoezi hilo kutumia
vizuri mafunzo waliyoipata kwenye zoezi hilo pindi wanapotakiwa kukabiliana na
matishio ya kiusalama na Majanga mbalimbali yanayoweza kutokea nchini, nchi
wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na duniani kwa ujumla.
Naye Kamanda Kikosi cha JWTZ wa zoezi hilo Luteni Kanali
Benard Mongela amemshukuru Mkuu wa Majeshi Jenerali Jacob John Mkunda kwa
kuwezesha kufanyika kwa zoezi hilo kwani washiriki wamepata fursa ya kubadilishana
uzoefu na wanajeshi wa EAC katika nyanja mbalimbali kama vile Ulinzi wa Amani,
kukabiliana na matishio ya Ugaidi, Uharamia na Majanga ya kibinadamu.
Zoezi Ushirikiano Imara 2024 lilifanyika kuanzia tarehe 6 hadi 23 Juni 2024 huko nchini Rwanda.
0 Maoni