Idadi ya waliofariki katika ajali ya moto iliyoua watoto
watatu wa familia moja jijini Arusha imeongezeka baada ya baba wa watoto hao
askari CRI wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Zuberi Hassan
Msemo naye kupoteza maisha.
Kaimu Kamanda wa Jeshi la Zima Moto na Uokoaji, Jeradi
Nonkwe, amethibitisha kutokea kwa kifo hicho, na kusema marehemu huyo alikuwa
ni baba wa watoto watatu waliofariki kwa ajali ya moto iliyotokea Juni 22,
2024.
Watoto waliofariki ni Mariam Zuberi (9), Salma Zuberi (7) na
Bisma Zuberi (3) ambapo mama wa watoto hao, Jasmine Khatibu (33), Mariam Mussa
(60), Mwanaid Aldina (50), Mussa Msemo (34), AbdulKarim Ramadhan (9) na dada wa
kazi aliyefahamika kwa jina moja la Ester (20) wanaendelea na matibabu.
Kamanda amesema kuwa baba huyo amefariki jana Jumapili Juni 23, 2024 wakati akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mount Meru jijini Arusha, na kueleza kuwa chanzo cha kifo chake ni kuvuta moshi mwingi alipokuwa akijaribu kuwaita watu waje wasaidie kuwaokoa.
0 Maoni