Tahadhari ya kimbunga hidaya Mashariki mwa Pwani ya Mtwara

 


TAARIFA KWA UMMA

UWEPO WA KIMBUNGA "HIDAYA" KATIKA BAHARI YA HINDI MASHARIKI MWA PWANI YA MTWARA

Dar es Salaam, 02 Mei 2024:

Kufuatia taarifa iliyotolewa jana tarehe 01 Mei, 2024 na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kuhusu uwepo wa mgandamizo mdogo wa hewa katika Bahari ya Hindi mashariki mwa pwani ya Mtwara, mgandamizo huo mdogo wa hewa umeendelea kuimarika na kuwa kimbunga "HIDAYA" chenye nguvu ya kati, kikiwa umbali wa takriban Kilomita 506 mashariki mwa pwani ya Mtwara.

Mwenendo wa mifumo ya hali ya hewa baharini inaonesha uwezekano mkubwa wa Kimbunga "HIDAYA", kusogea karibu kabisa na pwani ya Tanzania kuanzia usiku wa leo tarehe 02 Mei 2024 na kuendelea kuwepo hadi tarehe 06 mwezi Mei 2024. Hata hivyo, kimbunga hicho kinatarajiwa kupungua nguvu baada ya tarehe 6 Mei 2024.

Uwepo wa kimbunga "HIDAYA" karibu na pwani ya nchi yetu unatarajiwa kutawala na kuathiri mifumo ya hali ya hewa hapa chini ikiwa ni pamoja na kusababisha vipindi vya mua kubwa na upepo mkali katika baadhi ya maeneo ya mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani (ikijumuisha visiwa vya Mafia), Dar es Salaam, Tanga, Morogoro, visiwa vya Unguja na Pemba na maeneo ya jirani hususan tarehe 3 Mei 2024 kwa maeneo ya pwani ya kusini (Lindi na Mtwara) na kusambaa katika maeneo mengine ya ukanda wa pwani kuelekea tarehe 4 hadi 6 Mei 2024.

USHAURI: Wananchi katika maeneo tajwa na wote wanaojihusisha na shughuli mbalimbali baharini wanashauriwa kuchukua tahadhari kubwa na pia kuendelea kufuatilia na kuzingatia taarifa za utabiri na tahadhari kutoka TMA, na kupata ushauri na miongozo ya wataalam katika sekta husika ili kujikinga na athari zinazoweza kujitokeza. Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) inaendelea kufuatilia mwenendo wa kimbunga "HIDAYA" na athari zake kwa mifumo ya hali ya hewa hapa chini na itaendelea kutoa taarifa mara kwa mara kila inapobidi.

Imetolewa na: Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania.

Mawasiliano yote yaelekezwe kwa:

Mkurugenzi Mkuu, Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania, Chuo Kikuu cha Dodoma, Jengo la Utawala, Ndaki ya Sayansi za Kompyuta na Elimu Angavu, 1Mtaa wa CIVE, S.L.P 27, 41218 Dodoma; Simu: + 255 26 2962610: Nukushi: + 255 26 2962610 Barua pepe; met@meteo.go.tz; Tovuti: www.meteo.go.tz

(ISO 9001:2015 Certified in Aviation Services)

105A


Chapisha Maoni

0 Maoni