Mwanasiasa mkongwe nchini aliyeshirikiana na Baba wa Taifa
Hayati Mwalimu Julius Nyerere tangu enzi za TANU, Alhadji Mustapha Songambele, amempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuliongoza vyema taifa.
Mzee Songambele ametoa pongezi hizo mbele ya Katibu Mkuu wa
Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk Emmanuel Nchimbi, leo Jumamosi, Mei 25,
2024.
Balozi Nchimbi alikwenda nyumbani kwa Mzee Songambele
Mwananyamala jijini Dar es Salaam kumfikishia salam za pongezi kutoka kwa
Mwenyekiti wa CCM, Rais Samia kwa kuadhimisha miaka 99 ya kuzaliwa kwake.
“Mfikishie salam zangu mwambie anaongoza nchi vizuri
sana…nchi imetulia…nchi iko baridi kabisa hata chama nacho kimetulia mambo
yanakwenda vizuri kabisa,” amesema Mzee Songambele.
Ameongeza kusema kuwa iwapo mambo yangekuwa hayaendi vizuri,
basi pamoja na umri wake mkubwa, angeenda makao makuu ya chama kusema.
Kwa upande wake, Balozi
Nchimbi amesema Mzee Songambele alifanya kazi kubwa ya kujenga Chama na
Serikali tangu enzi za TANU na baadae CCM.
Mzee Songambele alizaliwa mwaka Mei 25,1925, mkoani Ruvuma
kabla ya kuhamia Magomeni, jijini Dar es Salaam, ambapo walikuwa miongoni kwa
watu waliompokea Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere jijini humo.
Alikuwa rafiki mkubwa wa Mwalimu Nyerere na ndiye
aliyemtafutia kiwanja Magomeni Mikumi ambako kuna nyumba ya Mwalimu, hivi sasa
ikiwa ni Makumbusho ya Taifa.
Aliwahi kushika nafasi kadhaa ndani ya Chama na Serikali, ikiwa ni pamoja na ukuu wa mkoa.
0 Maoni