Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limeipongeza Wizara
ya Maliasili na Utalii kwa ubunifu wa
kuvumbua bomu baridi lililoboreshwa kwa ajili ya kupambana wanyama
hatari kama Tembo kwa kushirikiana na
Shirika la Mzinga.
Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya
Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii, Mhe. Timotheo Mnzava wakati wa hafla maalum
ya Wizara ya Maliasili kupokea mabomu 4000 yaliyo tengenezwa na Shirika la Mzinga mjini Morogoro.
Mara baada ya kupokea mabomu haya Wizara ya Maliasili na
Utalii imeanza operesheni maalum katika Halmashauri 20 nchini na inaongozwa na Naibu
Katibu Mkuu CP Benedict Wakulyamba
"Naomba kutoa
pongezi za dhati kwa Wizara na Shirika kwa kuja na suluhisho hili na
natoa wito kwa halmashauri zinazoaumbuliwa na Tembo kununua na kutumia mabomu
haya ili kupambana na wanyama hao," amesisitiza Mhe. Mnzava.
Ameitaka Wizara kuendelea kutoa mafunzo kwa askari wa vijiji
na vijana kwa kuwa Serikali peke yake
haitaweza.
"Hii ni kazi ya sisi sote, Serikali peke yake haitaweza
ni lazima kuendelea kuwashirikisha
wananchi kwa kuwapa elimu," ameongeza.
Pia ameiomba Wizara kuendelea kufanya tafiti ili kubuni
mbinu nzuri zaidi za kukabiliana na changamoto hiyo kwa kuzingatia kuwa Tembo
wamekuwa wakizoea mbinu na kuendelea kuleta usumbufu.
Mwakilishi wa wabunge kutoka kwenye majimbo yenye changamoto
za Tembo walioshiriki hafla hiyo, Mhe. Salma Kikwete amempongeza Mhe. Dkt. Rais
Samia Suluhu Hassan na Wizara kwa kuendelea kutatua changamoto hii.
"Leo kila Mbunge amefurahi kwa kuwa hili ni jambo kubwa
ambalo litaleta suluhisho na sasa
tunakwenda kurudisha Salam kwa wananchi wetu kazi hii nzuri iliyofanywa
na wananchi," amesisitiza huku
akitaka elimu iendelee kutolewa.
Kwa upande wake, waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angelah
Kairuki amesema wizara yake itaendelea kutekeleza kikamilifu maelekezo ya
viongozi wakuu na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii.
Aidha, amesema uvumbuzi wa bomu hili baridi ni utekelezaji
wa maelekezo ya Mhe. Rais aliyoitaka
wizara kuja na ufumbuzi wa changamoto hiyo.
Ameeleza kuwa wizara yake itaendelea kuja na bunifu
mbalimbali kwa kuwa hakuna njia moja pekee ya kukabiliana na changamoto hiyo.
Ametumia jukwaa hilo pia kutoa pole kwa wananchi wote ambao wameathirika
kwa namna moja au nyingine.
Hafla hiyo pia iliwashirikisha wabunge, Naibu Katibu Mkuu C.P Benedict Wakulyamba, Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Ulinzi na menejimenti ya Wizara ya Maliasili na Utalii.
Na. John Mapepele
0 Maoni