Bunge laipongeza Wizara ya Maliasili kuvumbua bomu la kufukuza Tembo

 

Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limeipongeza Wizara ya Maliasili na Utalii  kwa ubunifu  wa  kuvumbua bomu baridi lililoboreshwa kwa ajili ya kupambana wanyama hatari kama Tembo kwa kushirikiana na  Shirika la Mzinga.

Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii, Mhe. Timotheo Mnzava wakati wa hafla maalum ya Wizara ya Maliasili kupokea mabomu 4000 yaliyo tengenezwa  na Shirika la Mzinga mjini Morogoro.

Mara baada ya kupokea mabomu haya Wizara ya Maliasili na Utalii imeanza operesheni maalum katika Halmashauri 20 nchini na inaongozwa na Naibu Katibu Mkuu CP  Benedict Wakulyamba

"Naomba kutoa  pongezi za dhati kwa Wizara na Shirika kwa kuja na suluhisho hili na natoa wito kwa halmashauri zinazoaumbuliwa na Tembo kununua na kutumia mabomu haya ili kupambana na wanyama hao," amesisitiza  Mhe. Mnzava.

Ameitaka Wizara kuendelea kutoa mafunzo kwa askari wa vijiji na vijana  kwa kuwa Serikali peke yake haitaweza.

"Hii ni kazi ya sisi sote, Serikali peke yake haitaweza ni lazima kuendelea   kuwashirikisha wananchi kwa kuwapa elimu," ameongeza.

Pia ameiomba Wizara kuendelea kufanya tafiti ili kubuni mbinu nzuri zaidi za kukabiliana na changamoto hiyo kwa kuzingatia kuwa Tembo wamekuwa wakizoea mbinu na kuendelea kuleta usumbufu.

Mwakilishi wa wabunge kutoka kwenye majimbo yenye changamoto za Tembo walioshiriki hafla hiyo, Mhe. Salma Kikwete amempongeza Mhe. Dkt. Rais Samia Suluhu Hassan na Wizara kwa kuendelea kutatua changamoto hii.

"Leo kila Mbunge amefurahi kwa kuwa hili ni jambo kubwa ambalo litaleta suluhisho na sasa  tunakwenda kurudisha Salam kwa wananchi wetu kazi hii nzuri iliyofanywa na wananchi," amesisitiza huku  akitaka elimu iendelee kutolewa.

Kwa upande wake, waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angelah Kairuki amesema wizara yake itaendelea kutekeleza kikamilifu maelekezo ya viongozi wakuu na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii.

Aidha, amesema uvumbuzi wa bomu hili baridi ni utekelezaji wa maelekezo ya Mhe. Rais aliyoitaka  wizara kuja na ufumbuzi wa changamoto hiyo.

Ameeleza kuwa wizara yake itaendelea kuja na bunifu mbalimbali kwa kuwa hakuna njia moja pekee ya kukabiliana na changamoto hiyo.

Ametumia jukwaa hilo pia kutoa pole kwa wananchi wote ambao wameathirika kwa namna moja au nyingine.

Hafla hiyo pia iliwashirikisha  wabunge, Naibu Katibu Mkuu C.P  Benedict Wakulyamba, Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Ulinzi na  menejimenti ya Wizara ya Maliasili na Utalii.


Na. John Mapepele 


Chapisha Maoni

0 Maoni